Search in This Blog

BABU ADAIWA KUNAJISI MJUKUU WA SIKU 45


MTOTO wa kike mwenye umri wa mwezi moja na nusu amelazwa katika Hospitali ya Wilaya ya Mpwapwa akiwa amechanika vibaya sehemu zake za siri huku akipata haja kubwa na ndogo kupitia sehemu moja.

Habari za awali ambazo zilipatikana zilidaiwa kuwa mtoto huyo alikuwa amenajisiwa na babu yake mzaa baba.

Akizungumza katika wodi namba saba ya hospitali hiyo mama mzazi wa mtoto huyo Regina Msemakweli (24), mkazi wa Kijiji cha Isingu alisema kuwa mtoto wake alimzaa Februari 25, mwaka huu akiwa njiani kuelekea hospitali kujifungua.

Alisema kuwa, Aprili 17, mwaka huu alikwenda kisimani na kumuacha mtoto huyo akiwa na mama mkwe na mtoto wake mwingine mdogo mwenye umri wa miaka miwili, lakini aliporudi kutoka kisimani alimkuta mtoto wake akilia bila kunyamaza.

Regina alisema kuwa baada ya kuona mtoto akilia bila kunyamaza aliamua kwenda kumuogesha ndipo aligundua sehemu za siri za mtoto huyo zikiwa zimechanika vibaya na alianza kutoa haja kubwa na ndogo kwenye sehemu ya haja ndogo.

Akizungumza kwa uchungu alisema kuwa hakuwa ameelewa kimetokea nini kwani hata mama mkwe wake hakusema kitu lakini madaktari baada ya kumchunguza mtoto walisema kuwa amebakwa.

“Nasikia tu na mimi kuwa watu wanasema amebakwa na baba mkwe wangu lakini wakati kitendo hicho kinatokea nilikuwa kisimani,” alisema.

Mganga Mkuu wa Hospitali ya Wilaya ya Mpwapwa, Dk Lunemo Sakafu alisema kuwa, mtoto huyo alifikishwa hospitalini hapo na walipomchunguza waligundua kuwa alikuwa akitoka haja kubwa na ndogo kwenye sehemu moja.

Daktari huyo amesema kwamba hizo ni dalili za kuingiliwa kwa nguvu kwa binti huyo. Alisema kuwa baada ya kufanya uchunguzi na kubainisha hayo walimwanzishia matibabu.

Hata hivyo Muuguzi Mkunga wa Hospitali ya Wilaya ya Mpwapwa, Mary Mgonela alisema kuwa, mtoto huyo na mama yake ambaye alisindikizwa na wifi yake alipokelewa katika hospitali hiyo siku nne zilizopita.

Alipohojiwa baba wa mtoto huyo yuko wapi alisema kwamba alikataa kwenda hospitalini kwa madai kuwa alikuwa anakwenda kuchunga ng’ombe.

Alisema kuwa baada ya kuonekana suala hilo ni gumu na lazima litolewe taarifa Polisi, wifi wa mama huyo alielekezwa kwenda Polisi kuchukua PF 3 lakini alipotoka hakurudi na wala Polisi hakufika.

Alisema kuwa baada ya wifi huyo kutoonekana ilibidi ripoti itolewe kwa daktari na kisha Polisi kwa ajili ya uchunguzi zaidi.

Alisema kuwa katika maelezo ya mama wa mtoto kabla ya kufika hospitali walianza kwenda kwa mganga wa kienyeji ambapo mganga huyo alimwambia kuwa hawezi suala hilo na ndipo walipoamua kuja hospitali.

Muuguzi huyo alisema kuwa, mtoto huyo ameumizwa vibaya na anaendelea kupatiwa matibabu huku madaktari wakijitahidi wanavyoweza kuokoa maisha yake.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma, Kamishna Msaidizi wa Polisi, David Misime alisema kuwa, hana taarifa juu ya tukio hilo na atalifuatilia.
 
Support : KARIBU TENA MDADISI MAM
Copyright © 2011. RISASI - Haki Zote Zimehifadhiwa.
KWA HISANI YA MDADISI MAMBO
Proudly powered by Blogger