Search in This Blog

"NITAWALIPUA VIGOGO WAUZA UNGA" MBUNGE

SAKATA la biashara ya dawa za kulevya limeibuka upya, baada ya Mbunge wa Mwibara, Kangi Lugola (CCM), kusema ataanika majina ya vigogo wanaofanya biashara hiyo haramu.

Akizungumza bungeni juzi, Lugola alisema anakusudia kupeleka bungeni majina ya viongozi wa taasisi za Serikali wanaojihusisha na biashara ya dawa za kulevya kabla ya kumalizika kwa mkutano huu wa Bunge.

Mbunge huyo pia aliwatuhumu viongozi hao wakiwemo mawaziri, kwa kuhusika na vitendo vya rushwa ama mihadarati.

Katika Bunge la tisa chini ya Spika Samuel Sitta, aliyekuwa Mbunge wa Viti Maalum, marehemu Amina Chifupa (CCM), aliwahi kutangaza kuwa yupo tayari kutaja hadharani watu wanaofanya biashara ya dawa za kulevya.

Amina ambaye kwa sasa ni marehemu, katika mchango wake bungeni alinukuliwa akisema. “Nitawataja hadharani kwa majina, hata kama ni mume wangu anauza dawa za kulevya nitasimama na kumtaja bila kuogopa.” Mohamed Mpitanjia aliyekuwa mume wake naye ni marehemu.

Katika kile kinachoonekana ni kufuata nyayo hizo, Lugola alisema kitendo cha viongozi wa juu serikalini kushindwa kuwataja na kuwachukulia hatua wafanyabishara hao licha ya kuwajua, ni wazi kuwa nao wanahusika.

Lugola alitoa kauli hiyo juzi, wakati akichangia Hotuba ya Makadirio ya Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu, inayoshughulikia Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI).

Katika mjadala huo, Lugola aliweka wazi msimamo wake wa kutounga mkono bajeti hiyo ya waziri mkuu, kutokana na sababu mbili, rushwa na dawa za kulevya.

“Ninawaomba wabunge wenzangu, kabla ya kumaliza mkutano huu wa Bunge nitakuja na orodha ya viongozi wa taasisi za Serikali, wanaojihusisha na madawa ya kulevya naomba mniunge mkono,” alisema.

Hata hivyo, Lugola alisema Kamishina wa Tume ya Kudhibiti Dawa za Kulevya, Christopher Shekiondo, anapaswa kuwajibishwa kwani ameshindwa kazi.

Lugola alisema biashara hiyo imezongwa na rushwa na kwamba hiyo ndiyo sababu inayomfanya Shekiondo ashindwe kuwakamata watu hao, licha ya kuwafahamu kwa majina.

“Kwa nini Shekiondo anatuambia anajua majina ya watu wanaofanya biashara ya kulevya, lakini hatutajii eti kwa kuwa wanashindwa jinsi ya kuwakamata.

“Hakuna cha kushindwa hapa kama sio rushwa nini, awajibishwe kama anashindwa kuwakamata, kwanini kama kuwakamata ni tatizo wasiombe msaada hata kwa FBI kama walivyoletwa juzi baada ya mauaji ya Padri,” alisema.

Alisema yeye hakubaliani na msemo wa Serikali wa vita dhidi ya dawa za kulenya, isipokuwa vita anayoinoa yeye ni vita ya rushwa.

“Kama viongozi hawa wameshindwa kuwakamata wahusika wanaosema wanawajua, basi wanahusika kuchukua rushwa au la sivyo, hata mawaziri na wenyewe wanahusika na biashara hiyo.

“Ninyi wabunge kama mnataka pesa zimiminike kwenye halmashauri zetu, tupambane na rushwa na dawa za kulevya,’ alisema.

Lugola alisema, Serikali haiwezi kupambana na rushwa bila kuwekeza fedha na kwamba isiwalaumu polisi kwa vitendo vya rushwa badala yake wawaongezee mishahara.

“Wafanyakazi wa Mamlaka ya Mapato (TRA), waliongezewa mishahara ili wasichukue rushwa kwa nini Serikali inapata kigugumizi kuongeza mishahara ya polisi?

“Mimi sitaunga mkono hoja hii kama Serikali haitaanzisha mfuko maalumu katika Jeshi la Polisi ili kuboresha maslahi yao,” alisema.

Mbunge huyo pia alilalamikia kitengo cha maafa kwa kudai kuwa kitengo hicho ni ulaji wa Serikali.

Alisema Serikali inasubiri wananchi wa jimbo lake wakumbwe na njaa ndipo wajenge miundombinu ya kilimo cha umwagiliaji kutoka Ziwa Victoria hadi Mwibara.

Mazishi ya vigogo yatengewa Sh bil. 1

Mbunge aliishangaa Serikali kutenga Sh bilioni 1 katika bajeti ya ofisi hiyo, kwa ajili ya mazishi ya viongozi wa kitaifa, huku huduma za wananchi zikizorota.

“Na hii Sh bilioni 1 iliyotengwa kwa ajili ya mazishi ya viongozi wa kitaifa, ni wizi mtupu, wabunge wenzangu tusukubaliane na maneno matamu ya bajeti hii,” alisema.

Kwa upande wake, Mbunge wa Nkasi Kaskazini, Ally Kessy (CCM) alisema wabunge wanapoteza muda kujadili bajeti ambayo sehemu kubwa imejaa ahadi za wafadhili.

“Hapa tunapiga kelele kupitisha bajeti tukienda kwenye halmashauri fedha hakuna, wafadhili hawajaleta, kwani tulidai uhuru kutegemea fedha za wafadhili?” Alihoji.

Aidha, alizitaka halmashauri zisiadhibiwe kwa kutopelekewa fedha, kutokana na ubadhirifu unaofanywa na watumishi wachache.

Alisema kuziadhibu halmashauri ni kuwaonea wananchi wasio na hatia kwa kosa la watendaji wachache waliopelekwa katika halmashauri na Serikali yenyewe.

Kessy pia alitaka Serikali kujenga uwanja wa ndege katika jimbo lake, ili kumaliza tatizo la maji na kujenga barabara zilizopo kandokando ya Ziwa Tanganyika kwa kuwa hali zake ni mbaya.

No comments:

Post a Comment

 
Support : KARIBU TENA MDADISI MAM
Copyright © 2011. RISASI - Haki Zote Zimehifadhiwa.
KWA HISANI YA MDADISI MAMBO
Proudly powered by Blogger