Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dk. Shukuru Kawambwa
 WANACHUO 435 wa mwaka wa pili katika Chuo cha Ualimu Bunda, mkoani 
Mara, juzi waligoma kula chakula cha jioni kutokana na madai mbalimbali,
 ikiwa ni pamoja na kubadilishiwa ratiba ya chakula kwa kutopikiwa wali 
kama ratiba ilivyokuwa inaonesha na badala yake wakapikiwa ugali.
Kufuatia hali hiyo, jana polisi wakiwa wamejiandaa kwa mabomu ya 
machozi na silaha mbalimbali walifika chuoni hapo kwa ajili ya 
kuimarisha ulinzi.
Aidha, Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya ya Bunda, chini ya 
uenyekiti wa Mkuu wa Wilaya, Joshua Mirumbe aliyewakilishwa na Katibu 
Tawala wa wilaya hiyo, Dominicus Lusasi ilifika chuoni hapo na kukutana 
na wanachuo hao ambao ni wa mwaka wa pili.
Katika kikao hicho iliamriwa kuwa kuanzia sasa ratiba ya chakula 
ifuatwe na wanachuo hao siku zinazoonesha ratiba ya kula wali wapikiwe 
chakula hicho.
Wakizungumza katika kikao hicho, waliyataja madai mengine kuwa ni 
kutorudishiwa kwa pesa zao walizotumia kununua vifaa vya kufundishia 
wakati wa mafunzo kwa vitendo.
Walisema kuwa wakati wa mafunzo kwa vitendo serikali ilikuwa 
haijaleta fedha za kununua vifaa vya kufundishia, hali iliyowalazimu 
kila mwanachuo kutoa fedha zake na kununua vifaa hivyo, ili kazi hiyo 
iende vyema.
“Tulitumia fedha zetu kununua vifaa vya kufundishia ili zoezi hilo 
liweze kwenda vizuri, lakini sasa tunashangaa hawataki kuturudishia,” 
alisema mwanachuo mmoja.
Walisema kuwa sasa wanautaka uongozi wa chuo hicho uwalipe fedha hizo
 kwani tayari wizara ilikwishazituma na kwamba kila mwanafunzi anatakiwa
 alipwe kiasi cha Sh 48,000.
Waliongeza kuwa, madai mengine ni pamoja na michango mbalimbali 
wanayodaiwa kuchangishwa, licha ya kuwepo waraka wa serikali wa kuzuia 
michango hiyo na kwamba sasa wanataka muafaka ili waweze kupewa fedha 
zao.
Alisema wamekuwa wakichangishwa Sh 5,000 za mahafali, lakini chakula 
wanachokula siku hiyo ni cha shule, wanafanyishwa kazi ya ulinzi, 
upasuaji kuni na mwaka jana pesa za chakula wakati wa mafunzo kwa 
vitendo zilikuwa Sh 50,000 kwa kila mwanafunzi lakini walipatiwa Sh 
14,500.
Kwa upande wake mkuu wa chuo hicho Josephat Rweyemamu alikanusha 
madai yote ya wanachuo hao na kusema kuwa fedha hizo za vifaa vya 
kufundishia wizara ilitoa agizo kuwa zinunue vifaa vya kufundishia na 
sio kuwapatia pesa taslimu wanachuo hao.
Hata hivyo, Katibu Tawala alimwagiza mkuu wa chuo hicho kuiandikia 
barua wizara kuhusu madai ya wanachuo hao kuhusu fedha zao walizonunua 
vifaa vya kufundishia ili waweze kurejeshewa.
 
 
 
 
 
 
No comments:
Post a Comment