Search in This Blog

MAGEREZA NCHINI YAFURIKA WAFUNGWA

Jeshi la Magereza limesema linakabiliwa na msongamano mkubwa wa wafungwa katika magereza yake na kwamba limeanza kupanga  mikakati ya kukabiliana na tatizo hilo.

Hayo yalisemwa jana na Kamishina Jenerali wake,   John Casmir Minja wakati akizungumza na waandishi wa habari katika sherehe za kuwatunuku nishani  maafisa na askari vyeo mbalimbali wa jeshi hilo zilizofanyika kwenye viwanja vya Magereza mkoani Shinyanga.

“Kweli kumekuwapo na msongamano katika magereza yote nchini kutokana na wafungwa kuwa wengi ikiwa kwa sasa idadi ya wafungwa 35,000 badala ya 29,552 hali ambayo imekuwa ni tatizo kubwa” alisema.

Katika hafla hiyo askari 43 wametunukiwa nishani mbalimbali kwa maafisa na askari wa vyeo tofauti      tofauti wakiwamo askari waliotumikia     jeshi hilo kwa muda mrefu.

Nishani hizo zilikuwa katika makundi manne maalumu ambayo ni nishani ya utumishi uliotukuka, utumishi wa muda mrefu Tanzania, utumishi wa muda mrefu na tabia njema na nishani ya Mwenge wa Uhuru daraja la nne.

Minja alisema hicho ni kitendo cha historia kwake cha kuwatunuku nishani hizo kwani lilikuwa ni jukumu la Rais Jakaya Kikwete kuwavisha siku ya sherehe za Muungano lakini aliamua kumpatia jukumu hilo.

Mmoja wa maafisa hao ambaye ni Mkuu wa Magereza kutoka mkoani Mwanza,  R. Mollel alitunukiwa nishani ya utumishi uliotukuka Tanzania na kueleza kuwa nishani hiyo ni furaha kwake kwa kulitumikia taifa na kuwa mzalendo ndani ya nchi yake ya Tanzania.

Maafisa na askari hao kutoka mikoa ya Mwanza, Mara, Kagera, Shinyanga, Geita na Simiyu nao walitunukiwa nishani hizo.
 
Support : KARIBU TENA MDADISI MAM
Copyright © 2011. RISASI - Haki Zote Zimehifadhiwa.
KWA HISANI YA MDADISI MAMBO
Proudly powered by Blogger