MANUSURA katika shambulizi la kigaidi
katika duka kubwa la Westgate jijini Nairobi Kenya, wamesimulia mkasa
mzima na kusema walivyoshuhudia wateja wenzao katika duka hilo wakiuawa
baada ya kubainika kutokuwa Waislamu. Wateja hao walisema walipangwa
mstarini na kuuawa baada ya kushindwa kukariri mistari ya Korani na hadi
jana watu 62 walikuwa wameuawa –wakiwamo Waingereza watatu – katika
mashambulizi ambayo kikundi cha kigaidi cha al Shabbab-chenye uhusiano
na al Qaeda- kinadai kuhusika.
Baadhi ya wateja walijificha ndani ya
stoo za duka hilo, huku wengine wakiingia kwenye makasha tupu ya bidhaa
au kujifanya wamekufa. Wengi walikuwa wakikimbia mauaji hayo yaliyokuwa
yakiwanyemelea baada ya kushuhudia wateja wenzao wakiuawa bila huruma
baada ya kubainika kutokuwa Waislamu.
Wanaume, wanawake na watoto walikuwa
wakipangwa na kuuawa kwa bunduki aina ya AK-47 baada ya kushindwa kutaja
jina la mama wa Mtume Muhammad au kukariri mistari ya Koran – hivyo
kuitwa makafir au wasio na imani.
Wengine walikimbia na kujificha ndani ya
maduka, benki na stoo wakati mabomu ya kurushwa kwa mkono yakilipuliwa
na risasi zikiwakosakosa.
Waliobahatika kunusirika walijitokeza
wakiwa wametapakaa damu huku wamejawa hofu, na majeruhi wakiondolewa nje
wakisukumwa kwenye vitoroli vya kununulia bidhaa dukani humo.
Mmoja wa manusura hao, Hannah Chisholm
(21), kutoka Haslemere, Surrey, alielezea hali ya kutisha na kuchanganya
iliyokuwa katika duka hilo, ambalo aliamua kulitembelea kama sehemu
yake ya likizo.
Alisema: “Tulikuwa tunakimbia huku na
huko lakini risasi zilikuwa zikiendelea kurindima hivyo tukaamua
kujificha katika chumba cha stoo idadi yetu tukiwa zaidi ya 60.
“Miongoni mwetu walikuwamo watoto na mtu
mwingine aliyekuwa amepigwa risasi. Awali tulidhani watu hao wenye
silaha walikuwa ni wezi, hivyo tuliamini kwamba wasingeweza kufika
mahali tulipokuwa.” Greg Aldous, kutoka New Zealand, alisimulia jinsi
alivyojificha kwenye kasha na kuona mtu akipigwa risasi umbali wa futi
30 kutoka alipokuwa.
Alisema magaidi hao “walikuwa wanaingia kutoka mlango wa mbele na wa nyuma nasi tulikaa kimya.”
Aliongeza: “Hawa ni Waislamu wenye
msimamo mkali. Walikuwa wakiua mtu yeyote. Wanatisha.” Baadaye aliweza
kutoroka kutokana na kiza hadi eneo la maegesho ya malori ya mizigo
ambako alikuta wengine wamejawa na hofu na wengine wakilia.
“Hisia zangu zilikuwa zinanituma
nijifiche, niliingia ndani ya kasha kubwa lililokuwa na katoni za bidhaa
za duka hilo na kujificha humo,” alisema.
“Nilinusurika mauaji hayo kwa sababu
niliondoka eneo la shambulio. Mtangazaji wa redio, Saadia Ahmed ni mmoja
wa watu 1,000 waliokimbia.
Alisema: “Nilishuhudia watu wachache
wakiinuka na kuzungumza Kiarabu na kisha magaidi hao kuwaachia. Rafiki
yangu alijitambulisha kuwa Mwislamu na kutamka neno kwa Kiarabu naye
akaachiwa. Kama wangeniona …mimi ni Mzungu, ningekufa. Wasingefikiria
mara mbili. Wanachukia rangi yako.”
Lakini akaongeza: “Niliona watoto wengi
na wazee wakiuawa. Sielewi ni kwa nini uue mtoto wa miaka mitano!
Walikuwa wakifyatua ovyo risasi kwa mtu yeyote aliyejaribu kutoroka.”
Mama mmoja, Kamal Kaur, ambaye alikuwa
akinunua bidhaa akiwa na familia yake, alituma ujumbe wa kushitua kwa
Twitter kuhusu tukio hilo alipofika nyumbani: “Nilishika nywele zangu na
kulia kwa huzuni kama mtoto. Damu ilitapakaa kichwani.
Haikuwa yangu. Yule mtoto mdogo
aliyekufa karibu yangu … Mwanangu wa kiume alinusurika kufumuliwa
kichwa. Risasi ilimkosa kwa inchi moja. Iligonga ukutani.
Iliporudi ilimpata mtoto mdogo wa kiume
aliyekuwa jirani yake ikamuua”. Mhandisi wa Mawasiliano ya Teknolojia,
Charles Karani (41), alisema:
“Nilijificha chini ya gari na binti
zangu, na niliona watu hao wakipanga watu wapatao 40 na kuuliza
waliokuwa Waislamu, na kama walikuwapo, ili kuthibitisha waliwataka
kutamka jina la mama wa Mtume Muhammad. Waliokosea walipigwa risasi.
Damu ilitapakaa kila mahali.
“Wanawake wawili waliokuwa chini ya gari
na mimi walikuwa na majeraha ya risasi miguuni. Wengine kwa uhakika
walikuwa tayari wamekufa.
Niliona wanne wamelala, hawatikisiki.
Bomu la kutupa kwa mkono lilirushwa na kuviringika hadi tulipokuwa.
Binti yangu akasema: ‘Baba, bomu hilo’-lakini tunashukuru Mungu
halikulipuka na nikalipiga teke likasogea mbali.”
Mwanamke mmoja, aliandika kwenye Twitter
kwa jina la Shirley Ghetto, akisimulia jinsi alivyojificha chini ya
magodoro dukani humo.
Aliandika akiwasiliana na watu: “ Je ni
salama kujitokeza? Kuna ukimya. Tafadhali naomba unijulishe hali
ilivyo.” Ofisa wa Umoja wa Afrika (AU), Fred Ngoga Gateretse, alitambaa
sakafuni na kuona magaidi hao wakifyatulia risasi wateja na polisi.
“Niaminini, watu hawa ni wadunguaji,” alisema. “Ni dhahiri kuwa wana mafunzo maalumu.”
Vikosi vya Kenya vilionekana vikiwa na
makombora wakati vikiingia katika duka hilo juzi baada ya helikopta za
Jeshi kupita juu ya duka hilo.
Awali maofisa wa usalama hawakusema
idadi ya watu waliokuwa wanashikiliwa mateka. Chama cha Msalaba Mwekundu
cha Kenya kilisema, kikikariri Polisi, kwamba watu 49 ndio
walioripotiwa kupotea.
Idadi hiyo bila shaka ndiyo iliyotumiwa
kama ya watu waliokuwa wanashikiliwa na magaidi hao. Wasio Waislamu ndio
hasa walikuwa walengwa wa shambulio hilo.
Msalaba Mwekundu juzi usiku uliongeza
kuwa idadi ya vifo iliongezeka kutoka 59 hadi 68 baada ya miili tisa
zaidi kupatikana katika operesheni hiyo ya uokoaji, lakini hata hivyo
jana Waziri wa Mambo ya Ndani wa Kenya, Joseph ole Lenku alisema idadi
ya waliopoteza maisha ni 62.
Awali ilisemekana kuwa magaidi hao
miongoni mwao walikuwa wanawake, ingawa Lenku alisema wote walikuwa
wanaume na baadhi yao walivalia kike. Tambo za al Shabaab Waasi wa
kiislamu walisema shambulizi hilo lilikuwa ni la kulipiza kisasi kwa
hatua ya Kenya kupeleka vikosi vyake Somalia mwaka 2011 kupambana nao.
Msemaji wa al Shabaab alisema kupitia
televisheni, kwamba watu kutoka Magharibi hawatakuwa salama nchini Kenya
hadi nchi hiyo iondoe vikosi vyake Somalia.
Alisema: “Wakenya wana damu viganjani mwao. Yeyote aliye tayari kuja Kenya anapaswa kujiandaa kukabiliana na hali halisi.
“Hatuogopi watu kutoka Ulaya na Marekani
kwa sababu sisi si dhaifu. Na tunawambia hao Wazungu, kwamba yeyote
ambaye amekuwa akisaidia waliokuwa wakitushambulia, waambieni Wakenya
kuacha mashambulizi yao kama wanataka kubaki salama.”
Al Shabaab ilisema kupitia mtandao wao
mpya wa Twitter- baada ya ule wa awali kufungwa Jumamosi-kwamba maofisa
wa Serikali ya Kenya walikuwa wanawataka watekaji kuzungumza nao.
“Hatutazungumza na Serikali ya Kenya
ilhali vikosi vyake vinavamia nchi yetu, hivyo kuleni matunda machungu
kutoka kwenye mavuno yenu,” al Shabaab iliandika. “ Kwa muda mrefu
tumepigana vita na Kenya ndani ya ardhi yetu, sasa ni wakati wa
kuhamishia vita ndani ya ardhi yao.”
Iliongeza: “Wakenya hawatajua uzito wa tatizo bila kuona, kuhisi na kushuhudia vifo kwa sura zote.”
Kenyatta ajibu Hata hivyo, Rais Uhuru
Kenyatta- ambaye amepoteza ndugu katika shambulizi hilo- alisisitiza
dhamira ya Serikali yake kuendeleza mapambano dhidi ya al Shabaab.
“Tulikwenda Somalia kusaidia kutuliza
nchi hiyo na la muhimu zaidi ni kupambana na ugaidi ambao umeiathiri
Kenya na dunia yote,” alisema. “Hatutaacha mapambano dhidi ya ugaidi.”
Alisema ingawa mashambulizi haya
yalifanikiwa, vikosi vya usalama vya Kenya vilishazuia mengine mengi.
Mapema juzi, Kenyatta (51) ambaye alichaguliwa miezi mitano iliyopita ,
alisema mwipwa wake na mchumba wake waliuawa katika shambulizi hilo
ambapo zaidi ya watu 175 walijeruhiwa wakiwamo watoto wengi.
Vikosi vya Kenya vilikuwa vikidhibiti
kamera zilizofungwa ndani ya duka hilo. Duka hilo ambalo ni maarufu na
linatumiwa na Wakenya matajiri na wataalamu wa kigeni, lilitapakaa miili
ya watu katika madimbwi ya damu.
Baadhi ya waliuawa wakiwa ndani ya
magari yao, huku wengine wakiondoka na majeraha makubwa. Wakanada
wawili, akiwamo mwanadiplomasia Annemarie Desloges, na wanawake wawili
wa kifaransa walithibitika kuwa miongoni mwa waliouawa, sambamba na
mshairi maarufu wa Ghana Kofi Awoonor.
Wizara ya Mambo ya Nje ya Marekani nayo
ilisema raia wanne wa nchi hiyo ni miongoni mwa waliojeruhiwa. Mlinzi wa
kampuni ya ulinzi ya binafsi, Jonathan Maungo aliiambia Reuters:
“Waliingia kupitia damu na ndivyo pia
watakavyoondoka.” Mtangazaji wa BBC, Anne Soy akizungumzia duka hilo
alisema: “Hili ni duka kubwa – ni moja ya maduka ya aina yake jijini
Nairobi. Mara zote huvutia wageni na Wakenya matajiri, wengi wakiwa ni
wenye asili ya India. Hali ambayo ni mtambuka kwa rangi, kabila na
uraia.”
Wateja wenye hofu walisimulia jinsi
walivyojificha na kuomba wasionwe na wanamgambo hao. Na pale njia
ilipoonekana kuwa wazi akina mama waliokuwa wakilia, walipakata watoto
wao wadogo na kutoka nje ya duka hilo la ghorofa nne na wanaume
waliotapakaa damu.
Katika mgahawa, mwanamke na mwanaume
walionekana wamelala chini wamekufa huku wamekumbatiana, kabla miili yao
haijaondolewa huku muziki katika mgahawa huo ukiendelea kusikika kwenye
redio. Nahashon Mwangi alikuwa kazini alipopokea simu kutoka kwa
mwanawe wa kiume, akimwomba amwokoe kutokana na kifo ambacho kilikuwa
kinamjongelea. “Baba, nimepigwa risasi shingoni na mkononi.
Navuja damu sana. Njoo unisaidie
tafadhali,” mwanawe huyo wa miaka 21 alisema. “Ilinichukua kama saa moja
hivi kufika eneo hilo,” Mwangi alisema. “Nilikuwa nalia nikiomba polisi
wamwokoe mwanangu. Nakumbuka kulia kama mtoto, nililia na kulia lakini
hawakuniruhusu kuingia.” Faraja ilimjia saa tano baadaye, pale mwanawe
huyo aliyejeruhiwa alionekana miongoni mwa watu waliopatikana na
kuokolewa na vikosi vya usalama vilivyokuwa vikipita duka baada ya duka.
Alikimbizwa katika hospitali ya Chuo Kikuu cha Aga Khan na kufanyiwa
upasuaji. “Naomba apone,” baba huyo mwenye mshituko alisema. “Kwa nini
watu hawa watufanyie hivi?” alihoji.
Mwathirika mwingine, mfanyakazi wa duka
hilo, Zipporah Wanjiru, akitoka kwenye kadhia hiyo akiwa hai lakini
mwenye mshituko alisema: “Walikuwa wakizungumza lugha fulani hivi ambayo
sikuwa naielewa, sikuelewa chochote – lakini sauti zao zilikuwa kali.”
Jana asubuhi al Shabaab ilituma ujumbe mwingine ukisema:
“Saa 14 za mapambano zimetumia risasi
1,400 na maisha ya watu 140 yatapotea kwa kulipiza kisasi. Asubuhi njema
Kenya!” Uliongeza kuwa walikuwa bado ndani ya duka hilo, wakipigana na
makafir wa Kenya ndani ya uwanja wao na kutangaza:
“Haki inapokataliwa, itadaiwa kwa nguvu.
Wakenya walikuwa salama katika majiji yao kabla ya kutuvamia na kuua
Waislamu.” Kikundi hicho cha magaidi kilidai kimeshaua zaidi ya Wakenya
100 makafir.
Msimamizi wa Mochwari ya Nairobi, Sammy
Nyongeza Jacob alisema miili ya Waafrika, Waasia na wenye damu
mchanganyiko wa Waasia na Wazungu ni miongoni mwa iliyofikishwa hapo
baada ya shambulizi hilo.
Mashambulizi ya awali Januari shambulizi
linaloaminika kufanywa na al Shabbab lilisababisha vifo vya watu watano
na watatu kujeruhiwa katika mgahawa ulioko Garissa, Mashariki mwa
Kenya, na Agosti mwaka jana mtu mmoja aliuawa na wengine sita kujeruhiwa
katika eneo la Eastleigh jijini Nairobi siku moja kabla ya ziara ya
aliyekuwa waziri wa zamani wa mambo ya nje wa Marekani Hillary Clinton.
Mwezi jana ofisi 18 za ubalozi wa
Marekani katika Mashariki ya Kati na nchi za Afrika zilifungwa baada ya
kupatikana ujumbe kati ya maofisa wa al Qaeda juu ya mipango ya kufanya
shambulizi kubwa la kigaidi na kulizuia.
Shambulio la duka la Westgate ni kubwa
kutokea nchini Kenya tangu lile la al Qaeda lililotekelezwa Afrika
Mashariki dhidi ya balozi za Marekani za Nairobi na Dar es Salaam
zilizolipuliwa siku moja huku Nairobi watu zaidi ya 200 wakiuawa mwaka
1998.
Mwaka 2002 kikundi hicho kilishambulia
hoteli ya Waisraeli ya Mombasa na kujaribu kutungua ndege ya Israeli
katika shambulizi lililopangwa.
-HABARI LEO