Dar es Salaam. Serikali imependekeza
marekebisho ya sheria ya kudhibiti dawa za kulevya itakayotoa hukumu ya
kifungo cha maisha na kufuta kipengele kwenye sheria ya sasa kinachompa
mshtakiwa nafasi ya kulipa faini.
Sheria iliyopo sasa ya Udhibiti wa Dawa
za Kulevya ya mwaka 1995 (Sura ya 95, Ibara ya 16) inasema, endapo mtu
atakamatwa kwa kosa la kumiliki, kusafirisha, kuzalisha au kutengeneza
mashine ya dawa za kulevya, atahukumiwa kifungo cha maisha jela au
kulipa faini ya Sh10 milioni.
Hatua hiyo inakuja wakati idadi ya Watanzania wanaosafirisha, kuzalisha na kutumia dawa hizo ikiongezeka hapa nchini.
Pamoja na mapendekezo hayo, wadau
mbalimbali wamesema kufanyika kwa maboresho hayo hakutasaidia kupambana
na tatizo lililopo hivi sasa, ikiwa maadili ya wananchi na viongozi
yaliyoporomoka hayatarekebishwa.
Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam
(UDSM), Dk Kitila Mkumbo alisema sheria yoyote itakayowekwa haiwezi
kuwa ‘mwarobaini’ wa kutibu tatizo la dawa za kulevya hapa nchini kama
wanaohusika hawatawajibishwa.
“Hivi sasa zipo sheria, lakini
hazitekelezwi. Kuna baadhi ya viongozi wakubwa kabisa wametajwa
kujihusisha na dawa za kulevya, lakini hakuna hatua zozote
zilizochukuliwa,” alisema Mkumbo.
Mbunge wa Kawe na Mjumbe wa Kamati ya
Katiba, Sheria na Utawala ya Bunge, Halima Mdee, alisema Tanzania ina
sheria nzuri na bora, lakini changamoto ipo katika utekelezaji wake kwa
kuwa rushwa ina mchango mkubwa katika kudhoofisha maendeleo ya taifa.
Mdee alisema ingawa sheria ya rushwa
iliyopo hivi sasa ni nzuri, ina kasoro kadhaa zinazohitaji kufanyiwa
marekebisho ili kuipa nguvu zaidi.
Alisema baadhi ya viongozi waliopewa dhamana na wananchi wanatuhumiwa kujihusisha na biashara ya dawa za kulevya.
“Kama mtandao wa dawa za kulevya
tunaousikia upo kuanzia viongozi wakubwa hadi wa chini, unadhani hata
ukiwa na sheria nzuri itatekelezwa na nani? alihoji Mdee.
Kamanda wa Kikosi cha Kuzuia na
Kupambana na Dawa za Kulevya nchini, Godfrey Nzowa alisema mapendekezo
ya sheria ya dawa za kulevya ni mazuri, lakini yana changamoto nyingi
katika utekelezaji wake.
Alisema ingawa sheria mpya
inayopendekezwa inataja adhabu ya juu kuwa ni kifungo cha maisha kwa mtu
anayejihusisha na biashara ya dawa za kulevya, haijaweka wazi kiwango
cha chini kwa mtuhumiwa atakayepatikana na kosa hilo.
“Kwa namna ilivyo sasa, sheria hii
inaweza kuleta shida kwa sababu haitaji ‘minimum sentence’ (kiwango cha
chini cha hukumu), hivyo mtu anaweza kusema mtuhumiwa afungwe mwaka
mmoja,” alisema Nzowa.
Nzowa alisema sheria ya dawa za kulevya
iliyopo inaweka kiwango cha chini cha adhabu kuwa kisiwe kifungo cha
chini ya miaka ishirini.
Mkurugenzi wa Kituo cha Sheria na Haki
za Binadamu (LHRC), Dk Hellen Kijo-Bisimba alisema kinachotakiwa si
sheria kali, bali viongozi wawajibike kwa kuwa kuna baadhi ya watu
walikamatwa na vidhibiti lakini wameachiwa huru.
“Sheria kali zitakuwa kwa ajili ya
wafanyabishara wadogo tu kwa sababu wale wakubwa wana fedha nyingi,
ndiyo maana tunahitaji viongozi kama Dk Harrison Mwakyembe (Waziri wa
Uchukuzi)wanaopambana, ingawa anaonekana kama anapigana na maji
yanayomrudisha nyuma,” alisema Dk Kijo-Bisimba.
Mmoja wa vijana walioathiriwa na dawa za
kulevya, ambaye hakupenda kutaja jina lake kwa sababu za usalama,
alisema sheria kali hazitasaidia chochote, kwa sababu wafanyabiashara
wakubwa ndiyo wanaotoa rushwa ili waendelee kufanya biashara hiyo.
“Kama kweli wanataka biashara ya dawa za kulevya iishe kabisa hapa nchini, waanze kwanza kutokomeza rushwa,” alisema.
Mwanamke mmoja ambaye ametumia dawa za
kulevya kwa muda mrefu, ambaye pia aliomba jina lake lisitajwe gazetini,
alisema sheria hiyo ni kali na kwamba kama itatekelezwa kikamilifu
‘mateja’ wengi ndiyo watakaopelekwa gerezani, kwa sababu wengi wao ni
maskini.
“Ninachoona sheria hii itaongeza viwango
vya kutoa rushwa kwa viongozi wasio waaminifu na kuwaacha watumiaji
wengi maskini wakiozea jela,” alisema.
Jitihada zaidi
Mbali na mapendekezo ya kuboreshwa kwa
sheria ya dawa za kulevya, Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera,
Uratibu na Bunge, William Lukuvi alisema Serikali pia imetoa mapendekezo
ya kuundwa kwa chombo maalumu kitakachokuwa na mamlaka kamili ya
kumshtaki mtuhumiwa.
“Tume ya Kuratibu Dawa za Kulevya haina
mamlaka kisheria ya kukamata, kukagua na kumfikisha mtu mahakamani na
badala yake majukumu hayo yako kwa Kikosi Maalumu cha Jeshi la
Polisi(Task force),” alisema.
Aidha, Lukuvi alisema mbali na kuwapo
kwa kikosi hicho kinachoshirikiana na tume kutekeleza majukumu hayo,
changamoto bado ni kubwa.
Mwananchi