Search in This Blog

MWANAJESHI ALIVYOMUUA KARUME KWA RISASI

Rais Abeid Amaan Karume pichani juu enzi za uhai wake.
MWANAJESHI aliyemuua Rais Abeid Karume kwa risasi Aprili 7, 1972 Luteni Hamud Mohamed Hamud, imeelezwa kuwa baba yake mzazi  mzee Mohamed Hamud alikuwa mpinzani mkubwa wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.
Mzee Hamud alikamatwa miezi michache baada ya Mapinduzi ya Januari 12, 1964 kwa tuhuma za kutaka kuipindua serikali mpya ya Karume. Alitiwa kizuizini na hatimaye kuuawa bila ya kushitakiwa.
Imeelezwa kuwa Luteni Hamud alifahamu juu ya kuuawa kwa baba yake miaka michache baadaye akiwa katika mafunzo ya kijeshi huko Tashkent, Urusi ya zamani. Inasemekana alitamka kwa kuapa kwamba, punde atakaporejea Zanzibar, angemuua Karume kulipiza kisasi cha kifo cha baba yake.
Kwa kupitia majasusi waliokuwa wanasoma na Hamud huko masomoni, yapo madai kuwa serikali ya Karume ilijulishwa juu ya kusudio la Hamud la kumuua Rais Karume, lakini haikuchukua hatua hata baada ya mwanajeshi huyo kurejea Zanzibar.
Badala yake, Karume alimpandisha cheo kuwa luteni katika sherehe iliyohudhuriwa na wakuu wa vikosi vyote vya ulinzi na usalama Zanzibar.
Je, taarifa juu ya ‘tamko’ la Luteni Hamud huko Tashkent juu ya dhamira yake ya kutaka kumuua Karume zilikuwa za uongo? Kwa alichokifanya ni dhahiri kwamba kilichosemwa na shushushu juu ya jambo hilo ni sahihi.
Mara baada ya Karume kuuawa , Hayati Thabiti Kombo Jecha  aliyekuwa Katibu Mkuu wa ASP na mmoja wa waliojeruhiwa vibaya katika shambulio la kumuua kiongozi huyo wa nchi amenukuliwa na Minael  Hossana Mdundo katika kitabu chake cha  Masimulizi ya Sheikh Thabit Kombo Jecha (Uk. 157/8) akieleza: “Mara ikapigwa risasi kutoka mlangoni, ikampiga Mheshimiwa Sheikh Karume shingoni.  Hapo hapo akaanguka akisema; “Hamad”… bahati mbaya risasi zote alizopigwa zilimpiga sehemu mbaya”.
 
Support : KARIBU TENA MDADISI MAM
Copyright © 2011. RISASI - Haki Zote Zimehifadhiwa.
KWA HISANI YA MDADISI MAMBO
Proudly powered by Blogger