JESHI la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam limepiga marufuku
ulipuaji wa fataki wakati wa sherehe za mkesha wa Mwaka Mpya, kutokana
na sababu za kiusalama.
Imeelezwa kwamba zuio hilo, linatokana na sababu za kiusalama na
matishio mbalimbali ya kigaidi katika ukanda wa Afrika Mashariki na
Kati. Hayo yameelezwa na Kamisha wa Polisi Kanda, Suleiman
Kova wakati akizungumza na waandishi wa habari jana ofisini kwake jijini Dar es Salaam.
Alieleza kuwa ikiwa itaruhusiwa, inawezekana kutumika kama mwanya kwa wahalifu, kutenda uhalifu wao.
“Kwa wale ambao wanapenda kusherehekea Mwaka Mpya kwa kulipua fataki
au fashi fashi, safari hii watafute mtindo mpya wa kusherehekea, lakini
fataki ni marufuku. Ieleweke hatufanyi kwa kumkomoa mtu, bali ni kwa
kuchukua tahadhari, sababu mtu anaweza akalipua fataki na mwingine
akatumia muda huo kufanya mambo yake na hasa kwa kuzingatia matishio
yaliyopo,” alisema Kamanda Kova.
Akizungumzia kuhusiana na usalama katika sherehe za Krismasi, alisema
ulinzi ulikuwa mkali na hakuna matukio makubwa ya uhalifu, yaliyotokea,
bali ni madogo ambayo hata hivyo waliweza kuyadhibiti.
Alisema kuwa
askari wa kituo cha Kigamboni, walitilia shaka gari aina ya Toyota
Cresta, lenye namba za usajili T607 BNE lililokuwa likiendeshwa na
Michael Joseph, mkazi wa Mjimwema, Kigamboni katika Manispaa ya Temeke.
“Tukio hili lilitokea Desemba 24 ambapo baada ya askari kutilia shaka
walilisimamisha na kuanza kulipekua, ambapo walifanikiwa kupata shotgun
yenye mitutu miwili na namba za usajili TZCAR 90774 iliyotengenezwa
China ikiwa imefichwa katika boneti ya gari karibu na injini,”
aliongeza.
Ndani ya gari hilo ilipatikana bastola moja aina ya Revolver, yenye
namba za usajili 393304379, ikiwa na risasi tano ndani ya kasha la
kuhifadhia risasi, iliyotengenezwa nchini Marekani.
Alisema pia zilipatikana risasi nyingine 11, ambapo risasi tisa kati
ya hizo ni za bunduki aina ya G-3 na risasi mbili za shotgun.
Alisema bastola nyingine yenye namba za usajili TZCAR 101489,
iliyotengenezwa Jamhuri ya Czech ilikamatwa juzi katika eneo la Madale
Kontena baada ya kutokea mtafaruku baina ya watu wawili.
“Huyu jamaa mtoa taarifa (Andrew Simon) alijeruhiwa na mtu
anayemfahamu kwa sura, akiwa anaendesha gari kisha kumsukuma nje ya gari
lake.
Baada ya mtoa taarifa kuhoji kilichotokea ndipo mtuhumiwa alikwenda
nyumbani kwake kisha muda mfupi alirudi na bastola mkononi. “Alipiga
risasi moja hewani na mbili zilimjeruhi mtoa taarifa katika ubavu wa
kushoto. Lakini tumeshajua bastola ni ya nani na tunafuatilia ili aweze
kukamatwa,” alisema.
Aidha, aliongeza kuwa kwa sasa polisi wanashirikiana na kampuni ya
ulinzi ya Kiwango ili kudhibiti wizi wa miundombinu katika minara ya
simu, ambapo kwa mwananchi atakayetoa taarifa atapata zawadi kuanzia Sh
100,000 mpaka Sh milioni moja, kulingana na uzito wa mafanikio
yaliyopatikana.
Alisisitiza wananchi waendelee kushirikiana na jeshi la polisi,
ambapo alitaja namba za Makamanda wa Mikoa ya Kipolisi ili wawape
taarifa moja kwa moja.
Kwa Dar es Salaam aliwataja Makamanda na namba zao za simu kuwa ni
Kamanda Marietha Minangi wa Ilala (0715 009 980), Kamanda wa Temeke
Engelbert Kiondo (0715 009 979) na Kamanda wa Kinondoni, Camillius
Wambura (0715 009 976).