Search in This Blog

OKWI KWENDA YANGA, RAGE ASEMA WAKULAUMIWA SI YEYE, SOMA HAPA KUMJUA

Dar es Salaam. Mwenyekiti wa klabu ya Simba, Ismail Aden Rage ameibuka na kusema kuwa lawama za kutokumsajili mshambuliaji wao wa zamani kutoka Uganda, Emmanuel Okwi zielekezwe kwa Kamati ya Usajili na Ufundi wa timu hiyo na wala siyo yeye.

Rage ambaye alikuwa nchini Marekani kwa mwezi mmoja akimuuguza mwanaye, alisisitiza kuwa Okwi alikwishauzwa kwa timu ya Etoile Du Sahel ya Tunisia na wala hakuwa wa Simba tena pamoja na wao kuendelea kudai fedha zao.

Alisema kuwa wakati anakwenda kumuuguza mwanaye, alikuwa amefanikiwa kusajili wachezaji wawili, Awadh Juma na Badru Ali tu, lakini huku nyuma bila ya kupata baraka zake, Kamati ya Usajili ilifanikiwa kumpa mkataba kocha mpya, Zdravko Logarusic kutoka Croatia na kusajili wachezaji watatu, makipa, Yaw Berko, na Ivo Mapunda na mlinzi Mkenya, Donald Musoti.

“Ikumbukwe kuwa Okwi alikuwa anakuja mara kwa mara hapa nchini, lakini kamati hizo hazikuona umuhimu wake, hawakufanya naye mazungumzo kujua nini kinachoendelea kuhusiana na timu yake ya Tunisia na sababu kubwa ya kufanya hivyo ni kutaka kunichafua mimi na kuonekana mbaya na adui kwa klabu ya Simba,” alisema Rage.

Alisema kuwa kilichokuwa kinazungumzwa muda wote ni kunitaka mimi kujiuzulu na kuwaachia madaraka, jambo ambalo haliwezekani kwani lazima wajue kuwa mimi ndiye mkombozi wa Simba.

“Nimefanya mabadiliko makubwa, kuanzia kuongeza kodi ya mapango yetu na klabu kuingiza fedha, kutoka kodi ya Sh200,000 mpaka sasa ya mamilioni, sasa watu wanataka kuona fedha hizo zinapotea na kuwatumia watu ili niondoke, nasema hili halitawezekana na kwa taarifa tu, wale wenye mipango ya kunivamia nyumbani, nimekwisha toa taarifa polisi na hatua kali watachukuliwa wakithubutu kufanya hivyo,” alisema.

Alisema kuwa njama nyingi zimefanyika katika suala la Okwi mpaka kujiunga na Yanga, lakini kwa sasa yeye anasimamia zaidi suala la malipo ya timu ya Etoile na mchakato huo unakwenda vizuri.

 “Hivi leo Mbwana Samatta akijiunga na Yanga au Azam FC, watanilaumu mimi, Okwi hakuwa mchezaji wetu, wana-Simba wajue hilo, kuzungumzia suala la Okwi na kunishutumu mimi ni kunionea tu, walipaswa kujua suala la fedha, nalo nimelizungumza sana na kutoa ufafanuzi, lakini kwa vile lengo lao mimi niondoke, wanaongea maneno mengi ya uzushi juu yangu… mimi ni kiongozi mwenye sifa na kujua mambo ya uongozi, siwezi kukurupuka kujibu suala lolote,” alisema.

Alisema kuwa suala la malipo ya Okwi siyo siri, kwani Kamati ya Utendaji inaelewa kuwa tumefungua kesi Fifa na kulipa Dola 10,000 ili malalamiko yetu yapangiwe jaji na kusikilizwa.

“Kuna barua ililetwa na Fifa kwa njia ya DHL, ilifika klabuni muda mrefu, barua hiyo ilikuwa na majibu ya Fifa na njia gani tufuate ili tuweze kupata haki yetu ya Dola 300,000 za Marekani, makusudi haikutiliwa mkazo, leo (jana) nimefanikiwa kulipa Dola 10,000 kutoka mfukoni mwangu na tunasubiri kusikilizwa kwa madai yetu,” alisema.
 
Support : KARIBU TENA MDADISI MAM
Copyright © 2011. RISASI - Haki Zote Zimehifadhiwa.
KWA HISANI YA MDADISI MAMBO
Proudly powered by Blogger