Dar es Salaam. Mwenyekiti wa klabu ya
Simba, Ismail Aden Rage ameibuka na kusema kuwa lawama za kutokumsajili
mshambuliaji wao wa zamani kutoka Uganda, Emmanuel Okwi zielekezwe kwa
Kamati ya Usajili na Ufundi wa timu hiyo na wala siyo yeye.
Rage ambaye alikuwa nchini Marekani kwa
mwezi mmoja akimuuguza mwanaye, alisisitiza kuwa Okwi alikwishauzwa kwa
timu ya Etoile Du Sahel ya Tunisia na wala hakuwa wa Simba tena pamoja
na wao kuendelea kudai fedha zao.
Alisema kuwa wakati anakwenda kumuuguza
mwanaye, alikuwa amefanikiwa kusajili wachezaji wawili, Awadh Juma na
Badru Ali tu, lakini huku nyuma bila ya kupata baraka zake, Kamati ya
Usajili ilifanikiwa kumpa mkataba kocha mpya, Zdravko Logarusic kutoka
Croatia na kusajili wachezaji watatu, makipa, Yaw Berko, na Ivo Mapunda
na mlinzi Mkenya, Donald Musoti.
“Ikumbukwe kuwa Okwi alikuwa anakuja
mara kwa mara hapa nchini, lakini kamati hizo hazikuona umuhimu wake,
hawakufanya naye mazungumzo kujua nini kinachoendelea kuhusiana na timu
yake ya Tunisia na sababu kubwa ya kufanya hivyo ni kutaka kunichafua
mimi na kuonekana mbaya na adui kwa klabu ya Simba,” alisema Rage.
Alisema kuwa kilichokuwa kinazungumzwa
muda wote ni kunitaka mimi kujiuzulu na kuwaachia madaraka, jambo ambalo
haliwezekani kwani lazima wajue kuwa mimi ndiye mkombozi wa Simba.
“Nimefanya mabadiliko makubwa, kuanzia
kuongeza kodi ya mapango yetu na klabu kuingiza fedha, kutoka kodi ya
Sh200,000 mpaka sasa ya mamilioni, sasa watu wanataka kuona fedha hizo
zinapotea na kuwatumia watu ili niondoke, nasema hili halitawezekana na
kwa taarifa tu, wale wenye mipango ya kunivamia nyumbani, nimekwisha toa
taarifa polisi na hatua kali watachukuliwa wakithubutu kufanya hivyo,”
alisema.
Alisema kuwa njama nyingi zimefanyika
katika suala la Okwi mpaka kujiunga na Yanga, lakini kwa sasa yeye
anasimamia zaidi suala la malipo ya timu ya Etoile na mchakato huo
unakwenda vizuri.
“Hivi leo Mbwana Samatta akijiunga na
Yanga au Azam FC, watanilaumu mimi, Okwi hakuwa mchezaji wetu,
wana-Simba wajue hilo, kuzungumzia suala la Okwi na kunishutumu mimi ni
kunionea tu, walipaswa kujua suala la fedha, nalo nimelizungumza sana na
kutoa ufafanuzi, lakini kwa vile lengo lao mimi niondoke, wanaongea
maneno mengi ya uzushi juu yangu… mimi ni kiongozi mwenye sifa na kujua
mambo ya uongozi, siwezi kukurupuka kujibu suala lolote,” alisema.
Alisema kuwa suala la malipo ya Okwi
siyo siri, kwani Kamati ya Utendaji inaelewa kuwa tumefungua kesi Fifa
na kulipa Dola 10,000 ili malalamiko yetu yapangiwe jaji na kusikilizwa.
“Kuna barua ililetwa na Fifa kwa njia ya
DHL, ilifika klabuni muda mrefu, barua hiyo ilikuwa na majibu ya Fifa
na njia gani tufuate ili tuweze kupata haki yetu ya Dola 300,000 za
Marekani, makusudi haikutiliwa mkazo, leo (jana) nimefanikiwa kulipa
Dola 10,000 kutoka mfukoni mwangu na tunasubiri kusikilizwa kwa madai
yetu,” alisema.