Search in This Blog

SASA NI ZAM YA WANAUME KUNYANYASWA KIJINSIA HUKO ZANZIBAR

HUKU mataifa duniani yakiendelea na siku 16 za kupinga udhalilishaji wa kijinsia, mambo yamegeuka Zanzibar ambapo wanawake wanadaiwa kuwanyanyasa wanaume.

Kwa ilivyozoeleka wanawake ndio waathirika wakubwa wanaokabiliwa na vitendo vya udhalilishaji, lakini hapa Zanzibar kibao kimewageukia wanaume ambao kwa mujibu wa jeshi la Polisi Mkoa wa Mjini Magharibi zipo kesi kadhaa zilizoripotiwa.

Akizungumza na Mwandishi huko Ofisini kwake Muembemadema, Mkuu wa Dawati hilo Staff Sagenti Zahor Faki, alisema kumekuwa na ongezeko kubwa la idadi ya wanawake wenye tabia ya kuwanyanyasa waume zao ikiwemo kuwapa vipigo.


Alisema dawati lake limepokea kesi tisa za wanawake kuwadhalilisha wanaume na kwamba kesi hizo zimeripotiwa kuanzia mwezi Januari mwaka huu hadi Oktoba.

Alisema wanawake wengi wenye kufanya vitendo vya udhalilishaji hasa vya kuwapiga waume zao, hufanya kwa kuvizia hasa wakiwa wanaume hao wamelala.

Mkuu huyo alisema sababu kubwa zinazopelekea waume hao kupigwa na wake zao zinatokana na wanawake wengi kuwa na wivu wa kupindukia katika ndoa zao pamoja na migogoro ya kugombani mali.

Aidha akizitaja sababu nyengine alisema zinatokana na watoto wakati wazazi wao wanapoachana huku mwanamke akizuia hati ya nyumba ambayo si haki yake bila kukaa kulitatua tatizo hilo.

"Sababu hii inatokana na mume alieachana na mke wakati wakiwa wameshazaa mwanamke huanza vurugu na kuzuia hati ya nyumba wakati si haki yake na husema hatoi mpaka apewe kitu fulani bila ya kukaa pamoja na kulitatua tatizo hilo", alifafanua Mkuu huyo.

Alifahamisha kuwa wanawake wengi wamekuwa wakiwavizia waume zao wakati wakiwa usingizini na kuwajeruhi sehemu mbalimbali za miili ikiwemo sehemu ya siri huku wakiwapa maneno makali.


Zahor alifahamisha kuwa mbali na malalamiko hayo lakini wanaume wengi wamekuwa hawaripoti katika Dawati hilo kutokana na mambo ya aibu jambo ambalo linawakosesha haki zao za msingi kama vile wanawake.

Hata hivyo Mkuu Zahor alisema hakuna hata lalamiko moja lililofikishwa mahakamani bali mengine huyatolea uamuzi na mengine bado yanaendelea na upelelezi.

Akizitaja changamoto zinazowakabili ni pamoja na wanawake wanaofanya vitendo hivyo kuja na hukumu zao mikononi jambo ambalo ni kinyume na sheria za nchi.

Hivyo aliwataka wanandoa kujua wajibu wao kwani ndoa ni hidaya huku akiwasisitiza kuacha tabia ya kuishi kwa chuki na kusikiliza fitna za watu ambao hawawatakii mema.

Pia aliwashauri wanaume hao kutoona tabu kufika katika vituo vinavyohusika ili viweze kuwatetea kama wananawake ambao hupaza sauti zao na kusikika haraka kutokana na kuundwa kwa tasisi mbalimbali kama vile Zafela, Tamwa na Dawati la kijinsia.

Kwa upande wake Naibu Katibu Mtendaji wa Jumuiya ya Maimam Zanzibar, Sheikh Khamis Yussuf Khamis akizungumzia saula hilo alisema ni kweli malalamiko hayo huwa yanaenda katika jumuiya yao.

Aidha alifahamisha kuwa jumuiya yao kesi hizo zinapotokezea huwa wanasuluhisha kwa kutumia njia za kidini hasa kuwapa wanandoa elimu ya kujua wajibu wao.

Hivyo aliwataka wanandoa hao kupata elimu ya kutosha kabla hawajafunga ndoa ili kuondokana na matatizo mbalimbali ya hapa na pale.

Sambamba na hayo aliwashauri vijana wa kiume kufuata mawazo ya busara kutoka kwa wazazi wao na sio kufuata utashi wa marafiki ambao hawawatakii mema katika ndoa zao.
 
Support : KARIBU TENA MDADISI MAM
Copyright © 2011. RISASI - Haki Zote Zimehifadhiwa.
KWA HISANI YA MDADISI MAMBO
Proudly powered by Blogger