Search in This Blog

AFISA WA POLISI MWIZI WA SHABA

Jeshi la polisi linamtafuta Ofisa wa Polisi anayehusishwa na wizi wa shehena ya madini aina ya shaba yenye thamani ya sh.mil 800 iliyokuwa ikipelekwa bandari ya Dar es Salaam
Maofisa wakuu wa jeshi hilo Mkoa wa Kipolisi wa Temeke, walikutana jana katika kikao cha kutafuta njia ya kumpata polisi huyo kwa kile kinachoelezwa kuwa baadhi ya maofisa wakuu wa jeshi hilo kupakwa matope katika kashfa hiyo.
Akizungumza na mwandishi wetu, Kamanda wa Mkoa wa kipolisi wa Temeke Engelbert Kiondo, alithibitisha kuwapo kwa kikao hicho, na kueleza mkutano huo ni mwanzo wa mchakato mzito wa kuchunguza jambo hilo na kumbaini Ofisa huyo anayetuhumiwa kwa wizi huo.
Alisema kuwapo kwa taarifa ya ofisa wa polisi kuhusika na kashfa hiyo kubwa, imewafanya kuwa na tahadhari kubwa katika kazi ya upelelezi, ambapo kwenye kikao hicho waliangalia hatua mbalimbali za kuzichukua ili kumtia mikononi polisi huyo.
"Tupo kwenye kikao na maofisa mbalimbali wa polisi kujadili suala hilo, jambo muhimu tunataka kumpata huyo polisi anayetuhumiwa kuhusika na wizi wa shaba pamoja na watuhumiwa wengine," alisema Kamanda Kiondo.
Polisi huyo mwenye cheo cha Mrakibu wa Polisi anadaiwa kushirikiana na askari mwenzake mwenye cheo cha koplo, baada ya kutuhumiwa kuonekana wakisindikiza lori lenye shehena hiyo ya shaba lililoibwa wakati likienda bandarini kwa ajili ya kusafirisha madini hayo kwenda nchi moja ya Ulaya.
Imeelezwa shaba hiyo ilikuwa ikitokea nchini Zambia na ilipakiwa kwenye makontena mawili kwenye lori namba T 755 BKZ na tela namba T 117 BMF mali ya kampuni ya Dhadho.
Aidha, shehena hiyo ya shaba ikiwa katika hali ya vipande 638, ilikamatwa na polisi ikiwa kwenye nyumba moja eneo la Mtoni Bank Club, huku baadhi ya vipande hivyo vikiwa katika mchakato wa kuhamishwa kwenda kwa wateja.
Hata hivyo, Kamanda Kiondo aliwataka wananchi kuwa na subira wakati wanachunguza tukio hilo, kwa kile alichosema kuna kila dalili watu waliohusika na wizi huo wana mtandao mkubwa hapa nchini na nje ya nchi.
"Kazi hii ni nzito, watu wanaohusika na wizi wana mtandao mkubwa kuanzia nchini Zambia hadi hapa nchini, tunatakiwa kuchunguza kwa makini ili watu wote wajulikane," alisema Kiondo.
Alisema kwa sasa wanawashikilia watu watatu wakihusishwa na tukio hilo,na alitaja majina yao kuwa ni Reginald Fabian Nyamilaga (38), Kassim Yusufu (23) na Dotto Juma Maloda (20).
DEREVA WA LORI ALIOKOTWA
Kamanda Kiondo alisema katika kitu kinachotia ugumu kwenye sakata hilo, ni baada ya kugundulika dereva wa lori hilo Goodluck Makundi hakuwa na nyaraka zinazoweza kumtambua.
Alisema kampuni ya Dhadho ambayo ilimuajiri, haikuwa na kumbukumbu kama inavyotakiwa katika sheria za ajira, kitu ambacho ni kigumu kutambua makazi yake na sehemu alipozaliwa.
Alisema pamoja na udhaifu huo, jeshi hilo linaendelea kumtafuta pamoja na mmliki wa yadi ya magari ilikohifadhiwa shaba hizo.
Jana jioni mwandishi wetu alipompigia simu Kamanda Kiondo baada ya kuzagaa uvumi kuwa, kigogo huyo (cheo na jina tunalo) na askari walioshiriki kwenye tukio hilo wanashikiliwa kituoni hapo, alisema kwa sasa ni mapema kulizungumzia.
Alisema hawezi kuthibitisha hilo kwa sababu habari wamezisoma kwenye moja ya magazeti nchini  na kwamba wanaendelea kuzifanyia kazi. 

No comments:

Post a Comment

 
Support : KARIBU TENA MDADISI MAM
Copyright © 2011. RISASI - Haki Zote Zimehifadhiwa.
KWA HISANI YA MDADISI MAMBO
Proudly powered by Blogger