Search in This Blog

WAJAWAZITO WA UPASUAJI DAR HATIHATI

 Ni baada ya umeme kukatika
Hospitali ya Sinza Palestina iliyoko Jijini Dar es Salaam, juzi usiku ililazimika kuwakimbiza haraka kinamama wajawazito kwenda Hospitali ya Mwananyamala kwa huduma ya upasuaji, baada ya umeme kukatika ghafla huku hospitali hiyo ikiwa haina jenereta.
Mwandishi wetu alifuatilia kituko hicho baada ya kupata taarifa kutoka kwa mmoja wa ndugu wa waliolazwa katika hospitali hiyo kwa ajili ya kujifungua.
Mtoa taarifa huyo ambaye hakutaka jina lake liandikwe gazetini, alisema juzi katika hospitali hiyo hapakuwa na umeme hali iliyosababisha mgonjwa wao kutokufanyiwa upasuaji kutokana na hospitali hiyo kukosa jenereta.
Alisema ameshangazwa na hali hiyo kwa hospitali ya kisasa kama hiyo kukosa jenereta inapotokea suala la dharura kama hilo.
Alisema wakati walipokwenda kumuangalia mgonjwa wao, walishtuka kujulishwa kuwa amehamishiwa hospitali ya Mwananyama kwa ajili ya upasuaji baada ya hospitali hiyo kushindwa kumfanyia kutokana na kukatika kwa umeme.
"Nilivyofika hospitali nikamkuta mume wa mgonjwa analia kwani alikuwa hajamuona mkewe akidhani atakuwa amefariki. Na tulipokuwa tunafuatilia tukaambiwa kahamishiwa hospitali ya Mwananyamala ili akafanyiwe operesheni kwani tatizo la umeme ndilo limesababisha upasuaji kutokufanyika," alisema.
Alisema kitendo cha kutokuwapo kwa jenereta katika hospitali hiyo ya Sinza, kunahatarisha afya za kinamama wajawazito. "Hivi kwa mfano ndio mtu anafanyiwa upasuaji halafu umeme unakatika ghafla hapo itakuwaje… kwa hiyo watamkimbizia Mwananyamala wakammalizie? Ni kwanini pasiwepo na jenereta umeme ukikatika kwani hata wagonjwa wanakuwa katika mazingira magumu," aliuliza.
Akiongea na gazeti hili, Mganga Mkuu wa Hospitali ya Sinza, Dk. Benedict Luoga, alikiri kuwapo kwa tukio hilo na kudai kuwa pamoja na kukosa jenereta pia ina uhaba wa watumishi.
Alisema juzi umeme ulikatika eneo lote la Sinza na hadi sasa (jana) haujarudi.
Dk. Luoga alikiri wagonjwa kutoka hospitali hiyo kupewa rufaa kwenda hospitali ya Mwananyamala kwa ajili ya huduma ya upasuaji.
Hata hivyo, alisema hospitali yake haitoi huduma ya upasuaji wakati wa usiku kutokana pia kukabiliwa na uhaba wa watumishi.
Alisema huo ndio utaratibu waliokubaliana na hospitali ya Mwananyama pale inapohitajika mama anapotakiwa kujifungua kwa upasuaji.
"Muda wa usiku kuanzia saa 2 huwa hatufanyi upasuaji kama atatokea mama anatakiwa kujifungua kwa njia ya operesheni basi tunampeleka Mwananyama na sio kwamba kukosekana kwa umeme ndio kumetufanya tuwapeleke wagonjwa katika hospitali hiyo," alisema.
Dk. Luoga alisema jenereta walilokuwa wakilitumia limeharibika na liko kwenye matengenezo.
Alisema wanahitaji jenereta kubwa ambalo litakuwa linatosheleza mahitaji ya jengo zima ambalo gharama zake ni Sh. mil 80.
Alisema suala hilo limewasilishwa katika ngazi ya Manispaa ya Kinondoni ili waweze kulifanyia kazi kwani jambo hilo lipo juu ya uwezo wake.
Mwandishi wetu hakuchoka bali ilimtafuta Mganga Mkuu wa Manispaa ya Kinondoni, Dk. Gunini Kamba ili aweze kulizungumzia suala hilo ambapo alisema kuwa tayari tatizo la jenereta ameliwasilisha kwa Mkurugenzi na kwamba linashughulikiwa.
Dk. Kamba alisema tatizo la uhaba wa wafanyakazi katika hospitali hiyo imetokana na ongezeko la wagonjwa kwani awali walikuwa wahudumu wachache na kwamba kwa sasa wanasubiri kibali cha ajira mpya.
Alisema katika hospitali hiyo inatakiwa kupelekwa jenereta jipya lenye ukubwa wa kukidhi mahitaji . 

No comments:

Post a Comment

 
Support : KARIBU TENA MDADISI MAM
Copyright © 2011. RISASI - Haki Zote Zimehifadhiwa.
KWA HISANI YA MDADISI MAMBO
Proudly powered by Blogger