POLISI mkoani Mbeya inamshikilia
mwanaume mmoja kwa kosa la kufanya mapenzi na mwanawe wa kumzaa.
Anayeshikiliwa ni mkulima na mkazi wa kijiji cha Syukula wilayani Rungwe
Asajile Mwamtina(46) ambapo anatuhumiwa kufanya tukio hilo Aprili 14
mwaka huu.
Kaimu Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa
Mbeya, Barakael Masaki alisema saa 12:00 za jioni Asajile alimvizia
mwanawe wa kumzaa mwenye umri wa miaka 13 aliyekuwa jikoni akiendelea
kupika na kisha kumshawishi kufanya naye mapenzi.
Alisema bila kujali utu na heshima
aliyopaswa kuonesha kwa binti yake, baba huyo alifanikiwa kufanya
mapenzi na mwanawe anayetajwa kuacha shule mwaka 2011 akiwa darasa la
tano kutokana na ugonjwa wa kifafa unaomsumbua.
Kwa mujibu wa Kaimu Kamanda Masaki,
wakati hayo yakiendelea mke wa mtuhumiwa ambaye ndiye mama mzazi wa
binti huyo, Tumikigwe Samalinga alikuwa safarini katika kijiji cha
Kiwira wilayani Rungwe kuuguza mgonjwa ambaye haijafahamika mara moja ni
nani katika familia hiyo.
Kutokana na tukio hilo, kamanda ameitaka
jamii kuacha tamaa mbaya za kimwili na kujiletea fedheha kwa jamii
sanjari na kufikishwa katika mkono wa sheria.
Wakati huo huo, vitendo vya kinyama
dhidi ya watoto vimeendelea kuibuka baada ya mkoani Mwanza, mwenye umri
wa mwaka mmoja na nusu kuuawa na watu wasiojulikana na kisha kukatwa
ulimi, mkono, mguu wa kushoto na kisigino cha mguu wa kulia na kuondoka
navyo.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Ernest
Mangu alisema mauaji hayo yamefanyika Aprili 16, mwaka huu saa 4.30
asubuhi katika kisiwa cha Maisome kijiji cha Kisaba, kitongoji cha
Lwabatele.
Mtoto huyo, Erick Msoma alipotea
nyumbani kwao tangu Aprili 10, mwaka huu katika kijiji cha Kahunda, kata
ya Katwe wilayani Sengerema kabla ya kubainika akiwa ameuawa. Polisi
inaendelea na upelelezi kubaini wahusika ili hatua za kisheria
zichukuliwe