Search in This Blog

BINTI WA MIAKA 16 ABAKWA MKOANI TANGA NA KUACHWA MTUPU


BINTI wa miaka 16 amebakwa na watu wasiojulikana hadi akazirai na wakamtelekeza katika nyumba mbovu akiwa hana nguo. Tukio hilo lilitokea Aprili 10, mwaka huu, ambapo binti huyo aligundulika asubuhi ya Aprili 11, mwaka huu na akina mama waliokwenda kutafuta maji ambapo walimwona binti huyo akiwa amezirai. Chanzo cha habari kilichoomba jina lake kuhifadhiwa kilisema binti huyo ambaye ni mkazi wa Muheza, alifika Korogwe takriban mwezi mmoja uliopita kwa lengo la kuishi na dada yake katika Mtaa wa Habitati, aliyefahamika kwa jina moja la Mariamu.


Baada ya kufika kwa dada yake, binti huyo alikuwa akilala katika chumba kimoja na watoto wenzake wa majirani katika nyumba wanayoishi na alichukua uamuzi wa kuwatoroka wenzake wakati wakiwa wamelala na kwenda mitaani alikokumbwa na mkasa huo.


Chanzo hicho kilisema binti huyo aligundulika kutokuwapo katika chumba alichokuwa amelala na wenzake saa nane usiku wa kuamkia Aprili 11, mwaka huu, ambapo hata dada yake alipowauliza wenzake asubuhi walimjibu hawafahamu alikokwenda.

“Wakati wenzake wakiwa wamelala ndipo alipotoka na hakuoenekana na dada yake alimuulizia asubuhi akitaka aamshwe akidhani amelala, akajibiwa hajulikani alipo na ndipo baadaye zikapatikana taarifa kuwa kuna binti ameonekana Mtaa wa Roma Kanisani,” kilisema chanzo hicho.

Habari zaidi zinasema kijana aliyekuwa na binti huyo usiku huo kabla ya kufanyiwa kitendo hicho amedai kumulikwa na tochi yenye mwanga mkali usoni, kisha akakabwa shingo na watu wanaodhaniwa kumbaka binti huyo kwa vile yeye alidai kufanikiwa kukimbia katika sakata hilo.

Mwandishi wa MTANZANIA alifika Hospitali ya Magunga Korogwe na kufanikiwa kumkuta binti huyo akiwa amelazwa kitanda namba 10 katika wodi ya wanawake mchanganyiko akiendelea kupatiwa matibabu huku akiwa na mama yake mzazi, Mwanaharusi Hassan (38).

Naye mama mzazi wa binti huyo, alisema mwanaye tangu kufikishwa hospitalini hapo amekuwa akipatiwa matibabu yenye kuridhisha, tofauti na habari zilizozagaa mitaani kwamba hasaidiwi.

Kwa upande wake, Mganga Mkuu wa Hospitali hiyo, Dk. Rashid Said, alisema tangu binti huyo afikishwe hospitalini hapo amepatiwa tiba stahili, huku vipimo vikiwa vimechukuliwa na majibu kupatikana ambapo hakuweza kukutwa na mbegu za kiume pindi alipopimwa.

“Vipimo vya maabara vinaonyesha kwamba mgonjwa hakukutwa na mbegu za kiume, sisi kazi yetu hapa tutaandika taarifa zetu na kuzijaza katika fomu namba tatu ya polisi na kuziwasilisha kwa wenzetu wa polisi kwa hatua zaidi kwa kuwa wao wanaweza kujua kama amebakwa,” alisema Dk. Said.

Naye, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tanga, Constantine Massawe, alithibitisha kutokea kwa tukio hilo na wanaendelea na uchunguzi wa kuwabaini waliohusika na tukio hilo.




chanzo - mtanzania
 
Support : KARIBU TENA MDADISI MAM
Copyright © 2011. RISASI - Haki Zote Zimehifadhiwa.
KWA HISANI YA MDADISI MAMBO
Proudly powered by Blogger