KIKOSI CHA M23
Msemaji wa Serikali ya Congo, Mende
Serikali ya Jamhuri ya Kidemokrasi ya
Congo imekanusha madai kuwa imejiondoa kwenye mazungumzo ya amani ya
Kampala baina yake na kundi la waasi la M23 ikisema waasi ndiyo
waliojiondoa kwenye mazungumzo hayo. Msemaji wa serikali ya Congo
Lambert Mende ameiambia sauti ya Amerika kuwa mazungumzo hayo
hayaendelei vyema kwa sababu waasi hao wanadai mambo yasiyowezekana.Mende alikuwa anajibu madai yaliyotolewa Jumapili na kiongozi wa M23 Betrand Bisimwa. Bisimwa aliimbia Sauti ya Amerika serikali haionyeshi nia ya kuendelea na mazungumzo ya Kampala na kwamba maafisa wake katika ujumbe wa Kampala wamerejea Kinshasa. Alisisitiza kuwa waasi wa M23 ndiyo waliojiondoa kwenye majadiliano na kwamba wajumbe wa serikali wangali Kampala.
Mwandishi wa idhaa ya Kiswahili ya Sauti ya Amerika Austere Malivika anasema baadhi ya wajumbe wa serikali wangali Kampala na kiongozi wa ujumbe huo waziri wa mambo ya nje Raymond Tshibanda alikutana na mpatanishi wa mazungumzo hayo kutoka Uganda siku mbili zilizopita baada ya kupitia Kampala akielekea Addis Ababa kutoka Kinshasa.
M23 hawajakanusha kuwa walikuwa na wajumbe wawili tu kwenye mazungumzo ya Kampala mwishoni mwa wiki. Wajumbe hao wamekutana mara mbili tu mwezi huu lakini mkutano huo sio wa moja kwa moja bali kupitia kwa mpatanishi wa Uganda.
Pande zote mbili zaonekana kutofautiana sana juu ya maswala nyeti. Bisimwa alisema Jumamosi ikiwa serikali haipo tayari kuwasamehe wapiganaji wa M23 ina maana kuwa haitaki amani na kwamba ikiwa serikali ya Kinshasa haitaki kuwajumwisha wapiganaji wa kundi hilo katika jeshi la kitaifa, hilo pia litakuwa tatizo kuu.
Mende alisema serikali ipo tayari kutoa msamaha kwa wapiganaji na kujumwisha wapiganaji wa vyeo vya chini katika jeshi, lakini sio makamanda wa kundi hilo. Alisema Kinshasa haiwezi kutoka msamaha wa jumla kwa kundi zima la M23 kwa sababu linajumwisha wahalifu wa kivita na wengine waliofanya ukatili na ukiukwaji mkubwa wa haki za binadamu. Chanzo: VOA