Viongozi
wa misikiti wametakiwa kutunza nidhamu katika nyumba hizo za ibada, na
kuachana na tabia ya kugombaniana uongozi, ili kuepusha migogoro
isiyokuwa ya lazima.
Wito huo umetolewa na Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Al-hajj
Maalim Seif Sharif Hamad katika hafla ya ufunguzi wa “Masjid Maulana”
ulioko Mwera, katika Wilaya ya Magharibi Unguja.
Amesema
misikiti ni nyumba za ibada, hivyo hakuna sababu kwa waislamu
kugombania misikiti, na badala yake viongozi watakaochaguliwa wawajibike
kutunza nidhamu na kuendeleza harakati za kiibada ikiwa ni pamoja na
kuendeleza darsa na mijadala ya kuuendeleza Uislamu.
Maalim
Seif amewataka waumini wa msikiti huo kushirikiana na kusaidiana katika
mambo mbali mbali ya kijamii, sambamba na kuchangia harakati za
misikiti kwa kuhakikisha kuwa wanasaidia kutatua kasoro zinazoweza
kujitokeza.
“Ipo misikiti inawaumini wengi wenye uwezo, lakini hufikia hatua ya
waumini kufanya ibada kizani kutokana na kukosa fedha za kununulia
umeme, au kuna mingine sehemu za vyooni hufungwa kwa muda mrefu kwa
sababu hali ya usafi hairidhishi”, alitanabahisha.
Amewahimiza
viongozi wa msikiti huo kuendeleza darsa ambazo zitasaidia kuwafunza
vijana maadili mema na kuweza kutekeleza ibada zao kwa uhakika.
Kwa upande wake Naibu Kadhi Mkuu wa Zanzibar Sheikh Hassan Ngwali,
amesema waislamu wana wajibu wa kuitunza na kuihifadhi misikiti, ili
iweze kuwa katika hali nzuri na usafi wakati wote.
Amesisitiza haja kwa waislamu kuitumia misikiti kwa shughuli za ibada na
elimu, na kuwataka viongozi kuwa mifano bora katika jamii juu ya
kuendeleza maadili ya kiislamu na ibada.
Makamu
wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Maalim Seif Sharif Hamad akisalimiana na
wananchi alipofika Mwera kwa ajili ya ufunguzi wa Masjid Maulana leo
Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Maalim Seif Sharif Hamad akifungua pazia kuashiria ufunguzi wa Masjid Maulana ulioko Mwera.
Makamu
wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Maalim Seif Sharif Hamad akikabidhi
funguo za msikiti kwa Mzee wa “Masjid Maulana” ulioko Mwera, Sheikh
Soud, katika hafla ya ufunguzi wa msikiti huo.