Search in This Blog

"WABUNGE WAKIKATAA KUIPITISHA BAJETI YA MWAKA HUU NITALIVUNJA BUNGE". KAULI YA SPIKA

 Spika wa Bunge Anne Makinda juzi usiku alifunga mjadala wa Bajeti Kuu ya Serikali, huku akiwaonya wabunge kwa kunukuu baadhi ya vifungu vya Kanuni za Kudumu za Bunge inayoashiria kuwa ikiwa hawatopitisha bajeti hiyo Rais atalivunja Bunge.

Akiahirisha kikao cha 53 cha Mkutano wa 11 wa Bunge unaoendelea mjini Dodoma juzi usiku, Spika Makinda alitaja Kanuni ya 107 (1) na (2) ambayo hutumika kukidhi matakwa ya Ibara ya 90 (2)(b) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inayohusu Rais kulivunja Bunge.

Kanuni hiyo ya 107.(1) inaeleza: “Mjadala kuhusu Hotuba ya Bajeti ya Serikali utakapomalizika, Spika atalihoji Bunge ili litoe uamuzi wake wa kupitisha au kutokupitisha Bajeti ya Serikali ili kukidhi matakwa ya Ibara ya 90(2) (b) ya Katiba.”

Akinukuu kifungu hicho cha Katiba, Makinda alisema: “Rais hawezi kulivunja Bunge, isipokuwa kama Bunge litakataa kupitisha bajeti.”

Mjadala wa Bajeti Kuu ya Serikali kwa mwaka 2013/14 umejadiliwa kwa siku nne kuanzia Jumatatu wiki hii ambapo Makinda alisema kuwa wote walioomba kuchangia walifanya hivyo wamekwisha.

“Nafunga mjadala wa Bajeti ya Serikali Kuu leo, wote walioomba na waliokuwepo wamekwisha,” alisema Spika Makinda.

Hata hivyo, wakichangia hotuba hiyo, wabunge wengi walionyesha kupinga bajeti hiyo katika maeneo mbalimbali ikiwamo misamaha ya kodi, ongezeko la kodi katika mafuta ya petrol na kodi ya umiliki wa laini za simu (Simcard).

Wabunge pia walipinga bajeti hiyo wakitaka sekta ya madini ichangie zaidi Pato la Taifa, kupitia na kurekebisha mikataba ya madini.

Hali hiyo huenda inazua hofu kuwa huenda wabunge wengi wakaipinga kwa kuipigia kura ya hapana.

Kifungu cha 107(2) cha Kanuni za Kudumu za Bunge inaelekeza kuwa uamuzi wa Bunge kupitisha au kutokupitisha Bajeti ya Serikali utafanywa kwa kupiga kura ya wazi kwa kuita jina la mbunge mmojammoja.

Jana Makinda alitangaza Jumatatu ijayo ya Juni 24 kuwa ndiyo siku ambapo wabunge watapiga kura kwa kuitwa majina mmojammoja ili kupitisha Bajeti ya Serikali au la.

Hata hivyo, kurejea kwa wabunge wa Kambi Rasmi ya Upinzani wa Chadema ambao hawakuchangia mjadala huo wa Bajeti Kuu ya Serikali, hata kuwasilisha Bajeti Mbadala, kunaongeza hofu kuwa huenda wabunge wote wa kambi hiyo wakaipinga.
 
Support : KARIBU TENA MDADISI MAM
Copyright © 2011. RISASI - Haki Zote Zimehifadhiwa.
KWA HISANI YA MDADISI MAMBO
Proudly powered by Blogger