DAR ES SALAAM. 
KAMATI ya Bunge ya Huduma za 
Jamii, imevikataa viwango vipya vya alama za ufaulu kwa elimu ya 
sekondari vilivyotarajiwa kuanza kutumika mwaka huu na kutaka utaratibu 
na alama zilizotumika mwaka jana, zitumike kupanga matokeo ya Mtihani wa
 Taifa wa Kidato cha Nne wa mwaka huu.
Serikali ilitangaza utaratibu mpya wa alama za 
Mitihani ya Kidato cha Nne na Sita kwa kufuta Daraja la Sifuri na kuleta
 Daraja la Tano.
                
              
Makamu Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Stephen 
Ngonyani  alisema jana kuwa kamati hiyo ilichukua uamuzi huo kwa kuwa 
pamoja na udhaifu ulio kwenye alama hizo, kamati yao haikuhusishwa 
katika mchakato wa kuandaa alama hizo. 
                
              
“Mwenyekiti wangu (Margaret Sitta) alisema kile 
hakiwezekani, kuna viwango ambavyo wameleta havipo kwenye nchi nyingine 
duniani, tumewaambia wakavifanyie kazi walete tena,” alisema mbunge huyo
 wa Korogwe Vijijini, ambaye ni maarufu zaidi kwa jina la Profesa Maji 
Marefu.
                
              
Ngonyani alisema waliagiza watendaji wa Wizara ya 
Elimu na Mafunzo ya Ufundi kuhakikisha wanaishirikisha kamati yao kwani 
imejaa walimu wanaoweza kushauri vizuri.
                
              
“Hatutaki watuletee mambo ambayo yamewashinda baada ya kuyapeleka kwa wananchi,” alisema Ngonyani.
                
              
Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya 
Ufundi, Profesa Sifuni Mchome akitangaza uamuzi huo mapema mwezi huu, 
alisema uamuzi wa kubadilisha mfumo huo umechukuliwa kutokana na 
changamoto zilizojitokeza mwaka 2012.
                
              
Alama zilizokuwa zikitumiwa awali na Baraza la 
Mitihani la Taifa (Necta), katika kupanga matokeo hayo, kwa Kidato cha 
Nne ni A=80-100, B=65-79, C=50-64, D=35-49, F 0-34 kwa upande wa Kidato 
cha Sita, A=80-100, B=75-79, C=65-74, D=55-64, E=45-54, S=40-44 na F= 
0-39.
                
              
Alama mpya zilizotangazwa ni A=75-100, B+=60-74, 
B=50-59, C=40-49, D=30-39, E=20-29 na F=0-19. Alama hizo ni kwa kidato 
cha nne na sita.
                
              
Kwa utaratibu huo, A ilitafsiriwa kuwa ni ufaulu 
uliojipambanua, B+ ni ufaulu bora sana, B ufaulu mzuri sana, C ufaulu 
mzuri, D ufaulu hafifu, E ufaulu hafifu sana na F ufaulu usioridhisha.
                
              
Katika utaratibu huo, mtihani wa mwisho 
ulitarajiwa kuwa na alama 60 na alama 40 zitokane na alama za Maendeleo 
ya Mwanafunzi Shuleni (Continuous Assessment-CA).
                
              
Mwaka jana baada ya Serikali kufuta matokeo ya 
mtihani wa Kidato cha Nne, Necta ilitumia CA ya 30 huku mtihani wa 
mwisho ukiwa na alama 70. MWANANCHI