Search in This Blog

“TUTAKILINDA CHAMA KWA NGUVU ZOTE NA HATUTAWAVUMILIA WASALITI” ……BAVICHA


Baraza la Vijana la Chama chama Demokrasia na Maendeleo (Bavicha), limesema litakilinda chama chao kwa nguvu na kwamba halitamvumilia atakayebainika kufanya vitendo vya kukihujumu.
 
Limesema kuwa uanachama ndani ya chama chao ni imani na siyo ushabiki, hivyo hawataruhusu mtu yeyote kuichezea hata kama mtu huyo atakuwa na umaarufu wa kupindukia.
 
Mwenyekiti wa Bavicha Taifa, John Heche, alitoa kauli hiyo jijini Mbeya wakati akihutubia mkutano wa hadhara katika viwanja vya Chuo cha Uhasibu (TIA).
 
Alisema kutokana na imani hiyo, wapo watu ambao wamekipigania chama chao na kulazimika hata kufungwa gerezani huku wengine wakipoteza maisha ili kuhakikisha Chadema inajengeka na kuwa imara, hivyo kitendo cha aina yoyote kinachoonekana kukihujumu chama hicho ni sawa na usaliti kwa wale waliokipigania.
 
“Mpaka hapa Chadema ilipofika kuna watu wameumia sana, wapo waliofungwa gerezani, wapo waliopoteza mali na wapendwa wao na pia wapo walikufa kwa kuipigania Chadema iwe imara, chama hiki hivi sasa ni sawa na imani, haturuhusu mtu mmoja au kikundi cha watu wachache waichezee imani yetu, tutakilinda chama chetu kwa nguvu zote na tunawahakikishia kuwa tutawapoteza wachache, lakini meli yetu itavuka salama,” alisema Heche.
 
Alisema kuwa Chadema hakijajengwa kwa umaarufu wa mtu mmoja, bali kimejengwa na imani ya wananchi wote, hivyo hata kama kiongozi wao yeyote wa juu akiwemo Mwenyekiti, Freeman Mbowe na Katibu Mkuu, Dk. Wilbrod Slaa, wakionyesha usaliti nao watatemwa ili chama kisonge mbele.
 
Alisema mpaka sasa Chadema kimeonyesha njia ya kweli ya ukombozi, mwelekeo na tumaini kwa Watanzania na ndiyo maana kila uchaguzi unapofika lazima kiongeze idadi ya wabunge, madiwani, wenyeviti wa serikali za mitaa na Vijiji.
 
 Aliongeza kuwa bila ya Chadema, uozo unaofanywa na Serikali ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) na ufisadi unaofanywa na viongozi wa CCM usingejulikana na Watanzania wangeendelea kuwa masikini wa kutupwa huku rasilimali za nchi zikizidi kutanufunwa na kikundi cha watu wachache.
 
Alisema kuwa hata maamuzi yaliyochukuliwa na Kamati Kuu ya chama hicho ya kumvua nyadhifa zote Naibu Katibu Mkuu, Zitto Kabwe na aliyekuwa Mjumbe wa Kamati Kuu, Dk. Kitila Mkumbo, ni maamuzi magumu yenye kutaka kujenga imani ya chama hicho kwa Watanzania. 
 
Alisema kuwa chadema kitaendelea kuchukua maamuzi kama hayo kwa kiongozi ama mwanachama yeyote atakayebainika kutaka kukiyumbisha kwa namna yoyote.

>>NIPASHE>>
 
Support : KARIBU TENA MDADISI MAM
Copyright © 2011. RISASI - Haki Zote Zimehifadhiwa.
KWA HISANI YA MDADISI MAMBO
Proudly powered by Blogger