Search in This Blog

“UCHAGUZI MDOGO WA MADIWANI KUFANYIKA FEBRUARI 27 MWAKANI”….NEC


Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) imetangaza kuwa uchaguzi mdogo wa kujaza viti vilivyo wazi vya madiwani katika kata 27 zilizoko katika halmashauri 23, utafanyika Februari 9, mwakani.

Mkurugenzi wa Uchaguzi wa NEC, Julius Mallaba, alisema jana kuwa viti hivyo vimekuwa katika kata hizo, kutokana na baadhi ya madiwani kufariki dunia na wengine kupoteza sifa.
Kata hizo na halmashauri zake kwenye mabano ni Segela na Mpwayungu (Chamwino),Ukumbi na Ibumu (Kilolo), Nduli (Iringa), Malindo (Rungwe), Santilya (Mbeya), Tungi (Morogoro), Mkwiti (Tandahimba) na Mkongolo (Kigoma).


Nyingine ni Sombetini (Arusha), Mrijo (Chemba), Magomeni na Kibindu (Bagamoyo), Mtae (Lushoto), Ubagwe (Ushetu), Namikago (Nachingwea), Partimbo na Loolera (Kiteto), Kiwalala (Lindi), Kilelema (Buhigwe), Kiomoni (Tanga), Kasanga (Kalambo), Rudewa (Kilosa), Kiborloni (Moshi), Njombe Mjini (Njombe) na Nyasura (Bunda).

Alisema uteuzi wa wagombea udiwani utafanyika Januari 15, wakati kampeni za uchaguzi zitaanza Januari 16 hadi Februari 8 na siku ya kupiga kura itakuwa Februari 9, mwakani.

Alisema zoezi la uwekaji wazi Daftari la Kudumu la Wapigakura litafanyika kuanzia Februari mosi, mwakani katika vituo walivyojiandikisha wapiga kura wakati wa Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2010 na kwamba, zoezi hilo litafanyika kwa siku saba.

Mallaba alisema wagombea wa udiwani watachukua fomu za uteuzi kwa msimamizi wa uchaguzi kuanzia Januari 2 kabla ya saa 10,00 alasiri.

Alisema wagombea wanatakiwa kuwasilisha fomu za uteuzi kwa msimamizi wa uchaguzi siku ya uteuzi katika muda muda usiozidi saa 10.00 alasiri.
 

CHANZO: NIPASHE
 
Support : KARIBU TENA MDADISI MAM
Copyright © 2011. RISASI - Haki Zote Zimehifadhiwa.
KWA HISANI YA MDADISI MAMBO
Proudly powered by Blogger