MBUNGE wa Kinondoni (CCM), Idd Mohamed Azzan, kwa
muda mrefu amekuwa akichafuliwa katika vyombo vya habari na hasa kwenye
mitandao ya kijamii, akitajwa kuwa mmoja wa wafanyabiashara wa madawa ya
kulevya lakini sasa amesafishwa.
Uamuzi wa Kamati ya Maadili ya Baraza la Habari Tanzania (MCT),
unamuweka Azzan pazuri, hivyo ni dhahiri kwamba mbunge huyo si
mfanyabiashara wa madawa ya kulevya, isipokuwa wabaya wake wamekuwa
wakimchafua kwa maneno ya rejareja.
MCT, iliagiza Azzan asafishwe na Gazeti la Raia Mwema, vilevile
limlipe fidia kwa sababu ndilo lililochapisha habari yenye kichwa cha
kuhoji Azzan ni mbunge au muuza madawa ya kulevya?
Uamuzi huo, ulifikiwa baada ya Kamati ya Maadili ya MCT, kupokea
malalamiko kutoka kwa Azzan, kupitia wanasheria wa Taasisi ya Haki
Kwanza, chini ya Wakili Kiongozi, Alloyce Komba.
MCT ilisikiliza pande zote mbili, yaani ule wa Azzan na Raia Mwema na kutoa uamuzi kwamba habari husika haikuwa imejitosheleza.
Hukumu hiyo ambayo nakala yake tunayo, inasema: “Gazeti limeshindwa
kuthibitisha kuwa liliongea na Azzan kabla ya kuchapa taarifa. Majibu
yanayodaiwa na gazeti kuwa ya Azzan, yalitoka katika chanzo tofauti bila
kuzungumza naye.”
Katika mapitio ya hukumu hiyo, MCT iligusia vipengele vinne ambavyo
vilionesha kwamba habari husika haikuwa imekamilika, hivyo uchapaji wake
ulikiuka misingi ya taaluma nzima ya uandishi wa habari.
Katika malalamiko ya Azzan, alilalamikia habari husika katika vipengele vitano ambavyo ni;
Mosi; ilikosa chanzo cha uhakika, sahihi na cha kweli.
Pili; hakupewa fursa ya kuulizwa ili naye ajieleze kwa upande wake.
Tatu; habari husika ilijaa maoni ya mhariri mwenyewe na mwandishi wake.
Nne; habari ilidanganya kuhusu mali alizonazo na jinsi ambavyo alizipata.
Tano; habari husika iliingilia haki yake ya kikatiba ya kuwa na uhusiano na watu wengine.
Pamoja na vipengele hivyo vitano, Azzan aliambatanisha maelezo kwenye
hati yake ya malalamiko kwenda MCT, akieleza kwamba habari husika
ilikiuka maadili na misingi ya uandishi wa habari ambayo inafafanuliwa
kwa kina kwenye Kanuni ya Maadili ya Wanahabari Tanzania hususan katika
ukurasa kuanzia wa pili mpaka sita.
Azzan alisema, muongozo kwa
wanahabari kama alivyosoma katika kanuni hizo ni kwamba habari lazima
iwe ya ukweli, uwazi, usahihi, kuhoji pande zote husika, kutokuwa na
ubaguzi wala upendeleo pamoja na kutokashifu.
Kutokana na hukumu hiyo, Azzan alizungumza na mwandishi wetu na
kueleza kufurahishwa kwake na uamuzi wa MCT kwa sababu umekuwa wa haki.
“Hili liwe wazi sasa kwamba sijihusishi na biashara ya madawa ya
kulevya, mimi mbali na uongozi nilionao kama mbunge, ni raia mwema
kabisa wa nchi hii,” alisema Azzan na kuongeza:
“Binafsi napambana na biashara ya madawa ya kulevya kwa sababu kati
ya vijana wanaoathirika, wengi wao wanatokea kwenye jimbo langu la
Kinondoni. Nataka kuhakikisha vijana wanakuwa salama dhidi ya matumizi
ya madawa ya kulevya.
“Sasa kama mimi mwenyewe napambana na hiyo
biashara, inakuwaje nituhumiwe? Najua kuna mtandao wa kunichafua,
binafsi sipo tayari ndiyo maana niliona hili ambalo Raia Mwema
wamelifanya inabidi nilishughulikie kisheria nisafishwe.”
Azzan aliendelea kusema kuwa kilichoandikwa kwenye habari husika
kilimshangaza kwa sababu kilitengenezwa kwa makusudi ili kuthibitisha
maoni kwamba yeye ni muuzaji wa madawa ya kulevya.
“Ilihojiwa eti
kwa nini naishi Magomeni, yaani wanataka ionekane kwamba mimi naishi
Magomeni ili niuze madawa ya kulevya, mbona watu wengi wanakamatwa
Kunduchi kwa biashara hiyo? Takwimu zinajionesha kuwa Kunduchi
imekithiri kwa madawa ya kulevya.
“Ilielezwa pia kuwa nyumbani kwangu kuna wasanii wengi maarufu huwa
wanakuja, hapa shabaha kuu ni kuuaminisha umma kwamba mimi nashirikiana
na wasanii kufanya biashara ya madawa ya kulevya. Huku ni kuniingilia na
kuvunja haki zangu kikatiba.
“Kwa nini niingiliwe haki zangu, kuwa
na uhusiano na watu wengi ni haki yangu ya kimsingi. Kama ninawasiliana
vizuri na wasanii maarufu ni mimi, haipaswi kugeuzwa vinginevyo. Kuishi
popote ndani ya nchi hii ni haki yangu mradi sivunji katiba,” alisema
Azzan.
Akaendelea: “Mambo mengi yaliwekwa kunichafua. Mfano, waliandika
habari bila hata kuwasiliana na mimi lakini ndani yake wakaweka maneno
ionekane mimi ndiye nimesema, haya ni makosa makubwa. Namna hii
waandishi wa habari wenyewe wanadhalilisha taaluma yao.
“Unafanyaje
udanganyifu mkubwa kiasi hicho? Unawaandikia Watanzania maneno ya uongo
ya kutunga halafu unasema hayo yametakwa na Azzan wakati mimi sijaongea!
Hii tabia siyo nzuri.”
Akikazia hilo, Azzan alisema kuwa ataendelea kubaki imara na wote
wanaopanga kumchafua watashindwa kwa sababu skendo wanayoitumia ya
madawa ya kulevya ni feki, maana hajawahi kujishughulisha na biashara
hiyo tangu azaliwe.
“Waendelee kunizushia lakini watashindwa, mimi
nipo imara sana, ingekuwa nafanya biashara hiyo pengine ningebabaika
lakini sitishiki kwa sababu mimi nipo safi, tena naamini hao wanaotunga
mambo ya kunichafua baadhi yao ndiyo wahusika wa chini kwa chini.
“Mimi ni mbunge na ninafanya biashara halali. Nilianza kuhangaika na
biashara zangu nikiwa kijana mdogo sana, nidhamu yangu ya kujituma
kutafuta na kutumia bila kufuja ndiyo imenifikisha hapa. Hawajui
nimehangaika kiasi gani kufanikiwa, naumia sana kuzushiwa.”