Search in This Blog

YANGA KWANUKA, YATIMUA BENCHI LAKE LOTE LA UFUNDI, SOMA ZAIDI HAPA

ufundi
Klabu bingwa ya soka Tanzania, Yanga imetimua benchi lake lote la ufundi kwa kile kilichoelezwa kuwa kushindwa kuleta matunda yaliyokusudiwa katika klabu hiyo.

Kutokana na hatua hiyo, Yanga imetangaza kujitoa katika mashindano ya Kombe la Mapinduzi yanayoanza leo huko Zanzibar.

Katibu Mkuu wa Yanga, Benno Njovu alisema jana kuwa klabu yake imechukua hatua hiyo ili kujipanga upya kwa michuano ya kimataifa pamoja na Ligi Kuu Tanzania Bara inayotarajiwa kuanza wiki tatu zijazo.

Msemaji wa Kombe la Mapinduzi, Farouq Karim alielezea kusikitishwa na hatua ya Yanga kujitoa katika michuano hiyo na kusema Ashanti ya Ilala imechukua nafasi ya timu hiyo.

Njovu alisema kuwa kutokana na kupewa notisi ya kutimuliwa; Kocha Msaidizi; Fred Felix “Minziro”, Kocha wa Makipa; Razak Siwa na Daktari wa Timu, Nassoro Matuzya, kwa sasa Yanga haina kiongozi wa benchi la ufundi.

Kocha Mkuu wa Yanga, Ernie Brandits alikwishatupiwa virago kwa kupewa notisi ya mwezi mmoja, siku chache baada ya kufungwa na Simba mabao 3-1 katika mechi ya Mtani Jembe kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Akizungumza jana, Siwa alisema: “Nakubaliana na uamuzi wa viongozi, siwezi kubishana nao kwa kuwa wao ndiyo wenye uamuzi wa mwisho kuhusiana na klabu.”

Njovu alisema kuwa kwa sasa uongozi unaendelea na mchakato wa kuwapata warithi watakaochukua nafasi hizo haraka ili waweze kuanza maandalizi ya mzunguko wa pili wa Ligi Kuu na Ligi ya Mabingwa Afrika baadaye Februari.

Yanga imepangwa kuanza ugenini na Komorozine ya Comoro kwa mechi za kwanza zitakazoanza kuchezwa kati ya Februari 7 na 9, mwaka huu.

Hata hivyo, Njovu alisema kuwa hadi kufikia jana, makocha 45 wametuma maombi ya kutaka kuinoa Yanga.

Simba uwanjani leo

Wakati hayo yakitokea Jangwani, Simba leo inashuka kwenye Uwanja wa Amaan, Zanzibar kupambana na AFC Leopards ya Kenya katika mchezo wake wa kwanza wa Kombe la Mapinduzi huku mgeni rasmi akiwa Kocha wa Mkuu wa Timu ya Taifa ya Italia, Cesare Prandelli.
Michuano ya Kombe la Mapinduzi ni sehemu ya maandalizi ya sherehe za kutimiza miaka 50 ya Mapinduzi ya Zanzibar na mwaka huu itashirikisha timu 12.
Mchezo huo wa Simba na Leopards utakaoanza saa 2:00 usiku, utatanguliwa na ule wa wenyeji KMKM ya Zanzibar ambayo itashuka kwenye uwanja huohuo, saa 10:00 jioni kuikabili KCC ya Uganda ikiwa ni mechi za Kundi A.
Mechi nyingine leo jioni kwenye Uwanja wa Gombani, Pemba, itazikutanisha Mbeya City na wenyeji Cloves Stars, ambayo ni kombaini ya Kisiwa cha Pemba.
Kaimu Kocha Mkuu wa Simba, Selemani Matola alisema jana kuwa kikosi chake kimejiandaa vizuri na matarajio ya kufanya vizuri leo.
“Timu yangu ipo tayari kwa mechi ya kwanza na kwa mazoezi tuliyofanya naamini tutaifunga Leopards na kujihakikishia nafasi ya kusonga mbele japokuwa tunaweza kukutana na ugumu, maana kama unavyoona kuna timu kutoka nje ya nchi hapa,” alisema Matola.
Naye beki wa Simba, Donald Mosoti ‘Musso’ alisema atahakikisha anawakaba vilivyo washambuliaji wa AFC Leopards, Allan Wanga na Jacob Kelly leo.

—MWANANCHI—
 
Support : KARIBU TENA MDADISI MAM
Copyright © 2011. RISASI - Haki Zote Zimehifadhiwa.
KWA HISANI YA MDADISI MAMBO
Proudly powered by Blogger