Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Philip Mulugo.
Serikali imewaagiza wakuu wa shule za sekondari nchini kuchukua hatua kali dhidi ya wanafunzi watakaobainika kumiliki simu za viganjani na kuwanyang’anya na kisha kuziteketeza kwa moto au kuzitupa chooni.
Agizo hilo lilitolewa na Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya
Ufundi, Philip Mulugo, wakati akizungumza na wananchi kwenye mkutano wa
hadhara uliofanika katika kijiji cha Totowe wilayani chunya.
Alisema sheria haiwaruhusu wala kuwapa haki wanafunzi kumiliki simu
wakiwa shuleni, hivyo mwanafunzi anayekwenda na simu shuleni anakuwa
amevunja sheria na taratibu za shule ambazo zinamzuia kumiliki na
kutumia masomoni.
“Nawaagiza walimu kuwa ukimwona mwanafunzi ana simu na kuitumia
nyakati za masomo, mnyang’anye na kuichoma moto au kuitupa chooni kwa
sababu wakati mwingine simu hizo wanakuwa wamenunuliwa na wapenzi wao na
hivyo kuwafanya washindwe kusoma vizuri na matokeo yake wanafeli
mitihani, sisi Wizara ya Elimu hatujaruhusu na wala hatufanyi hayo
mambo,” alisema Mulugo.
Alisema akitokea mzazi akalalamika au kumsumbua mwalimu kutokana na
kunyan’anya mwanae simu akiwa shuleni, maofisa watendaji wa vijiji na
mitaa wamchukulie hatua za kumkamata na kumpeleka Polisi ili afikishwe
mahakani.
Mulugo ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Songwe wilayani Chunya,
alisisitiza kuwa wanafunzi wakiachwa bila kudhibitiwa nidhamu zao, ndio
cha kushindwa kusoma na kupata matokeo mabovu kwenye mitihani ya kitaifa
na baadae kuharibikiwa kimaisha.
Alisema vijana ambao hawadhibitiwi nidhamu wawapo shuleni ndio
wanaoshindwa kufanya vema masomo yao na baadaye kuwa mzigo kwa taifa
kutokana na kujihusisha na mambo ya hovyo kama vile maandamano yasiyo na
tija, utumiaji wa dawa za kulevya na uhalifu mwingine kwenye jamii.
Aidha, Mulugo aliwataka walimu kuanza kutembeza bakora kwa
wanafunzi watukutu ili kuhakikisha nidhamu ya wanafunzi inarejea
mashuleni na kuwafanya watoto warejee kwenye masomo badala ya
kujihusisha na mambo ya hovyo.
CHANZO:
NIPASHE
No comments:
Post a Comment