Search in This Blog

WANAFUNZI 16,482 WALIOFAULU MTIHANI WA DARASA LA SABA WAKOSA SHULE ZA KUJIUNGA KIDATO CHA KWANZA

WANAFUNZI 16,482 waliofaulu mtihani wa darasa la saba mwaka huu wamekosa nafasi za kujiunga na kidato cha kwanza, kutokana na uhaba wa shule za sekondari nchini. Idadi hiyo ni kati ya wanafunzi 427,609 waliofaulu mtihani huo uliofanyika Septemba 11, katika maeneo mbalimbali nchini, ambapo wanafunzi 411,127 wamechaguliwa kujiunga na sekondari.

Matokeo hayo yalitangazwa jana jijini Dar es Salaam na Katibu Mkuu wa Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Jumanne Sagini, wakati akizungumza na waandishi wa habari.

Sagini alisema wanafunzi waliokosa nafasi wanatoka katika mikoa minane, ikiongozwa na Dar es Salaam yenye wanafunzi 11,796, Mbeya 1,484, Geita 1,578, Dodoma 549, Njombe 379, Morogoro 315, Katavi 261 na Mtwara 120.
Alisema wanafunzi waliokosa nafasi watasubiri hadi Februari mwakani, iwapo watapata shule katika uchaguzi wa awamu ya pili, kutokana na baadhi ya wanafunzi kwenda katika shule binafsi.

Haiwezi kuwa ni furaha kusema wengine wamepata na wengine wamekosa, tayari tumeziagiza halmashauri zilizobakiza wanafunzi kukamilisha ujenzi wa vyumba vya madarasa ili kuwawezesha wanafunzi hao kujiunga kidato cha kwanza ifikapo Machi, mwakani.

Hii si ya mara ya kwanza kwa wanafunzi wa darasa la saba wanaofaulu kukosa nafasi za sekondari, kwani mwaka jana baadhi ya wanafunzi waliofaulu mtihani huo katika mikoa ya Arusha, Njombe na Mwanza walikosa nafasi.

Katika Mkoa wa Arusha wanafunzi 6,838 walikosa nafasi, wakati Njombe ni wanafunzi 800 na Mwanza 1,400,” alisema.

Sagini aliwahimiza wazazi, walezi na viongozi wa wilaya husika kuhakikisha wanafunzi wote waliochaguliwa wanaandikishwa na kubakia shuleni hadi watakapohitimu elimu ya sekondari.

Katika hatua nyingine, Sagini alisema kuanzia sasa, mtoto yeyote atakayefika darasa la tatu kama atakuwa hana sifa za kuingia darasa la nne, atalazimika kurudia darasa.

Hatua hiyo inafuatia kuwepo kwa idadi kubwa ya wanafunzi wanaomaliza darasa la saba wakiwa hawajui kusoma, kuandika na kuhesabu.

Kulingana na matokeo ya utafiti yaliyotangazwa hivi karibuni na taasisi isiyo ya kiserikali ya Uwezo Tanzania (TWAWEZA), inaonyesha kuwa asilimia 24 ya wanafunzi wa darasa la saba hawawezi kusoma hadithi rahisi ya wanafunzi wa darasa la pili iliyoandikwa kwa lugha ya Kiswahili.

Utafiti huo pia ulibaini kuwa asilimia 50 ya wanafunzi hao hawawezi kusoma hadithi ya Kiingereza ya darasa la pili na asilimia 11 hawawezi kufanya hesabu rahisi za darasa la pili.

Taarifa nyingine iliyotolewa juzi na Chama cha Wamiliki wa Shule Binafsi (TAMONGSCO), ilieleza kuwa zaidi ya wanafunzi 12,000 waliofanya mtihani wa darasa la saba hawajui kusoma.
 
Support : KARIBU TENA MDADISI MAM
Copyright © 2011. RISASI - Haki Zote Zimehifadhiwa.
KWA HISANI YA MDADISI MAMBO
Proudly powered by Blogger