WANAFUNZI 16,482 waliofaulu mtihani wa darasa la saba mwaka huu wamekosa
nafasi za kujiunga na kidato cha kwanza, kutokana na uhaba wa shule za
sekondari nchini. Idadi hiyo ni kati ya wanafunzi 427,609 waliofaulu
mtihani huo uliofanyika Septemba 11, katika maeneo mbalimbali nchini,
ambapo wanafunzi 411,127 wamechaguliwa kujiunga na sekondari.
Matokeo
hayo yalitangazwa jana jijini Dar es Salaam na Katibu Mkuu wa Ofisi ya
Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Jumanne
Sagini, wakati akizungumza na waandishi wa habari.
Sagini
alisema wanafunzi waliokosa nafasi wanatoka katika mikoa minane,
ikiongozwa na Dar es Salaam yenye wanafunzi 11,796, Mbeya 1,484, Geita
1,578, Dodoma 549, Njombe 379, Morogoro 315, Katavi 261 na Mtwara 120.
Alisema wanafunzi waliokosa nafasi watasubiri hadi Februari mwakani,
iwapo watapata shule katika uchaguzi wa awamu ya pili, kutokana na
baadhi ya wanafunzi kwenda katika shule binafsi.
“Haiwezi kuwa ni
furaha kusema wengine wamepata na wengine wamekosa, tayari tumeziagiza
halmashauri zilizobakiza wanafunzi kukamilisha ujenzi wa vyumba vya
madarasa ili kuwawezesha wanafunzi hao kujiunga kidato cha kwanza
ifikapo Machi, mwakani.
“Hii si ya mara ya kwanza kwa wanafunzi
wa darasa la saba wanaofaulu kukosa nafasi za sekondari, kwani mwaka
jana baadhi ya wanafunzi waliofaulu mtihani huo katika mikoa ya Arusha,
Njombe na Mwanza walikosa nafasi.
“Katika Mkoa wa Arusha wanafunzi 6,838 walikosa nafasi, wakati Njombe ni wanafunzi 800 na Mwanza 1,400,” alisema.
Sagini
aliwahimiza wazazi, walezi na viongozi wa wilaya husika kuhakikisha
wanafunzi wote waliochaguliwa wanaandikishwa na kubakia shuleni hadi
watakapohitimu elimu ya sekondari.
Katika hatua nyingine, Sagini
alisema kuanzia sasa, mtoto yeyote atakayefika darasa la tatu kama
atakuwa hana sifa za kuingia darasa la nne, atalazimika kurudia darasa.
Hatua hiyo inafuatia kuwepo kwa idadi kubwa ya wanafunzi wanaomaliza darasa la saba wakiwa hawajui kusoma, kuandika na kuhesabu.
Kulingana
na matokeo ya utafiti yaliyotangazwa hivi karibuni na taasisi isiyo ya
kiserikali ya Uwezo Tanzania (TWAWEZA), inaonyesha kuwa asilimia 24 ya
wanafunzi wa darasa la saba hawawezi kusoma hadithi rahisi ya wanafunzi
wa darasa la pili iliyoandikwa kwa lugha ya Kiswahili.
Utafiti
huo pia ulibaini kuwa asilimia 50 ya wanafunzi hao hawawezi kusoma
hadithi ya Kiingereza ya darasa la pili na asilimia 11 hawawezi kufanya
hesabu rahisi za darasa la pili.
Taarifa nyingine iliyotolewa
juzi na Chama cha Wamiliki wa Shule Binafsi (TAMONGSCO), ilieleza kuwa
zaidi ya wanafunzi 12,000 waliofanya mtihani wa darasa la saba hawajui
kusoma.